Blog ya kijanja kwa ajili ya watu wajanja

Blog ya kijanja kwa ajili ya watu wajanja

Thursday, May 21, 2015

HISTORIA YA MUZIKI WA HIP HOP NA BONGO FLEVA NA JINSI UNAVYOONEKANA KUATHIRIWA ZAIDI NA WASHAIRI WA KIMAPOKEO KULIKO WANAUSASA

 Furaha Venance na Nganile Kyamba 
(Mwaka: 2015)

Katika makala haya tunakusudia kujadili namna muziki wa kizazi kipya (Bongo Fleva na Bongo Fleva) kuonekana kuathiriwa na wanajadi kuliko wanausasa. Hivyo basi ili kukamilisha hilo, kazi hii tumeigawa katika sehemu tatu. Sehemu ya kwanza ni utangulizi ambapo tutaangalia maana ya istilahi muhimu zinazojitokeza katika mada yetu, tutaangalia historia ya muziki wa kizazi kipya lakini pia tutaangalia kwa ufupi wanajadi na wanausasa ni vitu au mambo gani wanayoyasimia. Sehemu ya pili ni kiini cha swali letu, katika sehemu hii tutaangalia vipengele vinavyoonesha kuwa wasanii wa kizazi kipya kuathiriwa na wanajadi kuliko wanausasa na sehemu ya mwisho itakuwa ni hitimisho.

Maana ya Hip Hop na Bongo Fleva.
Wapo wanaouona muziki wa kizazi kipya yaani Hip Hop na Bongo Fleva kuwa ni kitu kimoja lakini wapo wanaopinga na kutofautisha kuwa Hip Hop na bongo fleva ni aina tofauti ya muziki (Omari 2009:5, Samwel 2012:12). Ama kuhusu neno Bongo Fleva mpaka sasa bado kuna utata kuhusu nani hasa mwasisi wa neno hili, inaelezwa kuwa, mwanamuziki wa regge, Jah Kimbute ndiye aliyeasisi neno hili pale alipoamua kuchanganya muziki wa asili na regge na kuziita Bongo Fleva. Mtayarishaji wa muziki P.Funk anaeleza kuwa mwasisi wa neno Bongo Fleva ni DJ Bonnie Love ambaye aliliasisi neno hilo mwaka 1998, Omari (keshatajwa, 10-11).

Madai haya kuhusu waasisi wa neno Bongo Fleva linaonekana kupingwa vikali na Mtangazaji wa siku nyingi, Michael Mhagama ambaye anadai kuwa yeye ndiye mwasisi wa neno hilo na aliliasisi katika kipindi chake cha DJ Show kilichokuwa kinarushwa na Redio One miaka ya 1990 hususani mwaka 1996. katika makala yake, Mhagama anasema, “Ilipofika dakika 30 za muziki wa R & B,siku hiyo nilikuwa kwenye usukani na kwa mbwembwe nilicheza nyimbo ya kundi la R&B lililoitwa 4Krewz Flava na baadaye kuiunganisha na nyimbo nyingine ya Unique Sistaz.Kwa vile midundo,mpangilio,lugha na utaalamu wa muziki wenyewe kamwe huwezi kuufananisha na ule wa Soul 4 Real au SWV kutoka Marekani,tulipenda tutofautishe kidogo kati ya aina hizi mbili na ndipo session hii niliibatiza jina ambalo lingetofautisha R&B ya Marekani na ile ya kwe tu….niliipa session hii jina la BONGO FLAVA.” Wengine wanaotajwa kuwa ni waasisi wa neno Bongo Fleva ni DJ. KBC, DJ. Phat Black, DJ. Venture na Steve B. (Reaster-Jahn na Hacke, 2014:24).

Ingawa lengo la kazi hii si kujikita katika mgogoro huo ila tumeona kwa umuhimu wake tuugusie japo kwa ufupi. Kama tulivyosema hapo awali kuwa wapo watu wanaouona muziki wa Hip Hop na Bongo Fleva kuwa ni muziki tofauti, Ramadhan Mponjika akinukuliwa na Samwel na wenzake (2013:55) anasema, muziki wa Bongo Fleva ni kapu ambamo ndani yake kuna miziki ya aina mbalimbali ikiwemo zouk, rhumba,regge, RnB, n.k. Kinachoelezwa hapa ni kuwa, muziki wa Bongo Fleva ni aina yoyote ya muziki wenye asili ya nje lakini unaimbwa kwa mahadhi ya Tanzania (Bongo) lakini si Hip Hop. Dai hili linaungwa mkono na Michael Muhagama (keshatajwa) kupitia andiko lake, anasema, “Hii ilikuwa mwaka 1996 na ndio ulikuwa mwanzo wa neno BONGO FLAVA likiwa na maana muziki wenye mahadhi ya nje lakini wenye vionjo na ladha ya Tanzania na si vinginevyo lengo kuu ni kuitofautisha na muziki ule wa Marekani. Hip Hop ya Tanzania ilibaki na itabaki vile vile kama ilivyo, ila muziki wowote ule wa nje, mbali ya Hip Hop na DANSI ya Tanzania niliuita na kuufahamishakwa umma wa watanzania kama BONGO FLAVA ndani ya kipindi cha DJ SHOW cha Radio One.” Hapa maana yake ni kuwa, jina la Bongo Fleva lilitumika tu, kutambulisha muziki wenye asili ya nje lakini wenye mahadhi ya Tanzania (Bongo) tofauti na muziki wa Hip Hop na dansi ambayo yenyewe ilitambulishwa kwa jina la Hip Hop ya Tanzania/Bongo au Bongo Hip Hop.

Ama kuhusu Hip Hop, Mahenge (2011:8) anasema, Hip Hop ni aina ya ushairi, usimuliaji au usemaji unaopangwa kivina kwa kufuata mdundo wa ala za muziki ambao ulisharekodiwa. Pamoja na kwamba fasili hii ya Mahenge inatupa mwanga kuhusiana na maana ya Hip Hop ambayo kwa kiasi kikubwa tunakubaliana nayo lakini dai la kusema usimuliaji au usemaji unapangwa kivina kwa kufuata mdundo wa ala za muziki ambao ulisharekediwa si sahihi kwani sasa hivi wasanii wengi wa Hip Hop wanaimba juu ya midundo ya muziki ambayo haijarekodiwa vyombo vya muziki vinapigwa sambamba na wao wakiimba na wakati mwingine hurap kwa mtindo unaojulikana kama mitindo huru yaani kutoa mashairi ya papo kwa papo kwa kufuata midundo ya muziki inayopigwa au bila kuwepo kwa midundo ya miziki yaani akapela.

Kwa maoni yetu, tunaona kuwa Hip Hop na Bongo Fleva ni muziki tofauti, muziki wa Hip Hop ni utamaduni unaombatana na elementi za, michoro, rap, Dj, mabreka, ni muziki ambao mashairi yake yanaganwa kwa kutumia mashairi yenye vina na midundo mizito wakati bongo fleva ni mkusanyiko wa muziki wenye asili kutoka nje ya Tanzania lakini yenye mahadhi na vionjo vya Tanzania ambayo hujumuisha Zouk, Kwaito, RnB, Kwaito, n.k. Kwa ujumla muziki huu Hip Hop na Bongo Fleva huitwa kwa jina la muziki wa kizazi kipya ikiwa na maana ya muziki unaopendwa na vijana kizazi cha sasa (Omari 2009:5, Samwel 2012:12).

Historia ya muziki wa kizazi kipya (Hip Hop na Bongo Fleva)
Muziki wa Hip Hop tunaarifiwa kuwa uliasisiwa na Wamarekani wenye asili ya Kiafrika katika mji wa Bronx huko New York katika miaka ya 1970 (Omari, keshatajwa:1). Nchini Tanzania unakadiliwa kuwa uliingia miaka ya 1980 Omari (keshatajwa), Mwanjoka (2011), Mbilinyi (keshatajwa), Reuster-Jahn (2014). Katika kipindi hiki vijana wengi hususani wale waliotoka katika familia zenye uwezo walianza kuimba mashairi (muziki) ya rap kwa kuiga nyimbo zilizokuwa zikiimbwa na wanamuziki wa Marekani wakati huo. Chachage aliwahi kuandika kuwa, katika mazingira hayo ndipo baadhi ya vijana waliokuwa wakijitambulisha kwa kusikiliza muziki wa  Reggae  wa Bob Marley na kucheza  ‘Break Dance’  katika miaka ya 1980, ili kujinusuru na kuyasahau matatizo yao, walipoanza kujipambanua na muziki wa  Hip Hop (Bongo Fleva). Mwanzoni ulikuwa ni muziki ulioambatana na kuiga kisisisi muziki huo. Kuiga kisisisi maana yake kuiga kitu kama kilivyo.

Madai haya ya kuiga muzuki wa Marekani yanaungwa mkono na Mwanjoka (keshatajwa, 8) anaposema, “Mbali na kuiga nyimbo, vijana hao wa Tanzania waliingiwa na mapenzi ya ndani  zaidi na muziki huo hata kujikuta wakiiga mavazi, mitindo ya nywele, mienendo hadi kuongea toka kwa wanamuziki hao wa Marekani na Ulaya.”

Hivyo tunaona kuwa wasanii wa Hip Hop na Bongo Fleva mwanzoni walianza kuimba kwa kunakiri na kukariri mashairi ya wasanii hao wa nje na hata midundo waliyokuwa wanaitumia ilikuwa ni midundo hiyo hiyo ya wasanii wa nje. Mbilinyi (keshatajwa, 32) anaongezea kwa kusema kuwa, “Kama kulitokea na aliyerap kwa kutumia lugha ya Kiswahili basi alitumia flow (kutiririka) ya nyimbo za mamtoni zilizokuwa maarufu kama ambavyo alikuwa anafanya mkongwe Saleh Jabir katika nyimbo kama Ice Ice Baby ya Vanilla Ice na OPP ya Naught by Nature ilikuwa ndiyo staili ya kipindi hicho.” Ufafanuzi katika mabano ni wetu.

Lakini baadaye wasanii wakaachana na uigaji wa muziki wa kimagharibi na kuanza kutunga nyimbo zao binafsi kwa lugha ya Kiswahili na Kiingereza jambo linaloendelea mpaka sasa ingawa tungo za Kiswahili ndiyo hupewa nafasi kubwa. Na msanii wa kwanza kabisa kuanza kuandika na kuimba kwa Kiswahili alikuwa ni Salehe Jabir ambaye kwanza tunaelezwa kuwa alianza kubadilisha nyimbo za Kiingereza kwa kutumia Kiswahili zilizotamba kipindi hicho na baadaye akaanza kutunga nyimbo zake mwenyewe. Hapo ndipo ikachochea wasanii wengi kuona kumbe inawezekana kurap kwa Kiswahili ndiyo nao wakaanza kujitokeza kutunga na kuimba kwa lugha ya Kiswahili, Mbilinyi (keshatajwa) na Mwanjoka (Keshatajwa).

Baadhi ya wasanii na makundi ya Hip Hop wanaotajwa kuwa ni waasisi wa muziki huu walikuwa ni, Fresh XE, BBG, Adili Kumbuka, Salehe Jabir, KBC, Samia X, The BIG, Rymson, 2 proud (Sugu), makundi ni kama vile, Kwanza Unit, Deplowmatz, HardBlasterz, Gang Stars With Matatizo (GWM), Wagumu Weusi Asilia, Young Da Mob, Afro Reign, Jungle Crewz Pose, Bantu Pound, Hardcore unit kwa kutaja machache. Wasanii na makundi ya kuimba (Bongo Fleva) ni kama vile, Mawingu Band, Lady Jay Dee, Stara Thomas, Unique Sisters, Nurueli, 4Kruz kwa kutaja wachache Mhagama (keshatajwa), Mbilinyi (keshatajwa), Mwanjoka (keshatajwa).

Aidha kabla hatujaingia katika kiini cha mjadala wetu, tuwaangalie kwanza wanajadi na wanausasa ni mambo gani wanayoyasimamia na kuyasisitiza katika utungaji wa mashairi. Ushairi wa kijadi ni ushairi unaozingatia urari wa vina na mizani kuwa ndiyo  roho na uti wa mgongo wa mashairi ya Kiswahili kwao hawataki kukiri kuwa mashairi yalaiyotungwa katika mtiririko (masivina) ni mashairi (Mulokozi na Kahigi, 1979:1) kwa maana hiyo kwa pamoja na vipengele vingine katika ushairi wa jadi ni kuzingatia vina kama anavyotuambia Abeid (1952:viii), “Neno moja tukumbuke katika utungaji, nalo ni hili ya kuwa mawazo ya mtungaji yazue vina, siyo vina kuzua mawazo.”

Madai haya yanaonekana kuungwa mkono na wanajadi wengine kama vile, Chirahdin, Mayoka, Kandoro, Al-amin Mazrui na Ibrahim Shariff kuwa vina na urari wa mizani ndiyo vitambulisho vya ushairi wa Kiswahili (Mulokozi na Kahigi, 1979:11). Jambo la msingi hapa ni kuwa wanajadi wanakumbatia sana suala la vina na mizani katika tungo za mashairi. Ili kuwa na shairi zuri, mwanajadi Sheikh Amri Abeid anataja mambo manne muhimu yanayopaswa kuzingatiwa katika ushairi ambayo ni, mizani, vina, kituo na kujitosheleza. Wanajadi wengine wanaotaja mambo muhimu yanayotakiwa kuzingatiwa katika ushairi ni pamoja na, Massamba (1983) anataja vina, mizani, kituo, muwala, Kibao (1983) naye anataja, mizani, vina, urari, muwala, utoshelevu na kuwa na maana wakati Komba (1977) anataja, mizani, vina, kituo na utoshelevu. Ama kwa hakika tukiwachunguza wataalamu hao tutagundua kuwa, wanachosisitiza shairi lenye sifa za ujadi linatakiwa kuzingatia vipengele vifuatavyo, Mizani, vina, kituo na kujitosheleza.

Kwa upande wao, wanausasa wanaona shairi si lazima lifuate urari wa vina na mizani, Mathalani, Mulokozi na Kahigi (1982;25) wanasema ushairi ni sanaaa inayopambanuliwa kwa mpangilio maalum wa maneno fasaha na yenye muwala kwa lugha ya mkato, picha, sitiari au ishara katika usemi maandishi au mahadhi ya nyimbo, ili kuleta wazo au mawazo, kufunza au kueleza tukio au hisi fulani kuhusu maisha au mazingira ya binadamu kwa njia inayogusa moyo. Kwa maoni yao wanausasa wanaona kuwa shairi ni sanaa yenye mpangilio mzuri wa maneno, lugha ya mkato na matumizi mengine ya lugha ili kutoa mawazo wao hawasisitizi juu ya kuzingatia urari wa vina na mizani kama wafanyavyo wanajadi.

Hivyo basi tukiwaangalia mambo yanayosisitizwa na wanajadi na wanausasa, tunakubaliana na hoja kuwa, muziki wa Hip Hop na Bongo Fleva unaonekana kuathiriwa zaidi na wanajadi kuliko wanausasa. Na vipengele ambavyo wanajadi wanasisitiza kuzingatiwa katika ushairi ambavyo vinaonekana kujitokeza katika mashairi ya Hip Hop na Bongo Fleva kama tulivyoona hapo awali ni, Mizani, vina, kituo na kujitosheleza. Hebu tuangalie vipengele hivyo namna vinavyojitokeza katika mashairi ya Hip Hop na Bongo Fleva ambavyo ndivyo vinavyotufanya kushadidia hoja hii kuwa muziki wa kizazi kipya unaonekana kuathiriwa na wanajadi kuliko wanausasa tukianza na;

Vina, tunaelezwa na Amri Abeid (1952:4) kuwa ni silabi za namna moja zinazotokea baada ya kila mizani kadha katika mstari wa shairi. Kwa upande wake, Wamitila (2003:345) anasema vina ni, dhana inayotumiwa katika taaluma ya ushairi kuelezea silabi zinazofanana katika sehemu sawa katika mpangilio wa ubeti wa shairi. Anaendelea kufafanua kuwa shairi linaweza kugawika katika vipande viwili na kuwa na vina vya kipande kimoja na kipande kingine. Hiki ndiyo kipengele kinachoonesha kuwa wasanii wengi wa muziki wa kizazi kipya (Hip Hop na Bongo Fleva) kwa kiasi kikubwa kuonekana kuathiriwa na ujadi.

Kati ya vitu ambavyo wanajadi wanasisitiza katika mashairi ni urari wa vina na mizani, kwa mfano Mnyampala (1962: Dibaji) anasema, Ushairi ni msingi wa maneno ya hekima tangu kale. Ndicho kitu kilicho bora sana katika maongozi ya dunia kwa kutumia maneno ya mkato na lugha nzito yenye kunata iliyopangwa kwa urari wa mizani na vina maalumu kwa shairi. Hapa Mnyampala pamoja na kuongelea suala la shairi kutumia maneno ya mkato na lugha nzito lakini maneno hayo yanatakiwa kupangwa kwa urari wa vina na mizani. Suala la urari wa vina pia linashadidiwa na Shabaan Robert ( 1958) akinukuliwa na Massamba (1983:54) janaposema, Ushairi ni sanaa ya vina inayopambanuliwa kama nyimbo, mashairi na tenzi.Zaidi ya kuwa sanaa ya vina ushairi una ufasaha wa maneno machache au muhtasari.

Kama tulivyoona kwa wanajadi, vina ni kigezo kinachozingatiwa sana na wasanii wa Hip Hop/Bongo Fleva katika tungo zao. Hiki ndicho kigezo ambacho kwa asilimia kubwa ndicho kinatufanya kushadidia hoja hii kuwa mashairi ya Hip Hop na Bongo Fleva yanaonekana kuathiriwa sana na wanajadi kuliko wanausasa. Katika muziki huu, wasanii wasiozingatia matumizi ya vina katika tungo zao zinaonekana hazina maana kama wanajadi wanavyoona kuwa mashairi yasiyozingatia vina kuwa si chochote, kama anavyosema Afande Sele katika wimbo wake wa Mtazamo;
 Au wengine mmetumwa kama mamluki,
 maana yake hamna maana mnarap mradi rap,
 mistari imekosa vina yenye vina haina maana.

Aidha katika wimbo wake mwingine, Darubini Kali Afande Sele, anawashangaa wasanii wenzake wanaoimba bila vina kama anavyosema,
Mi nacheka sana kuna vitu vya kuimba vyenye maana kila kona,
(Sasa) inakuwa vipi unataja taja majina tu nyimbo nzima
Tena kwa mistari isiyo na vina!

Kwa mtazamo wa Afande Sele msanii asipozingatia matumizi ya vina anaonekana kama mamluki na mtu asiye na maana kwenye sanaa. Kwa wasanii wa muziki wa kizazi kipya hususani wa Hip hop, matumizi ya vina yanasisitizwa zaidi na hata wengine kujinasibisha kuwa wao ni wataalamu wa kutumia vina kama anavyojinasibisha Solo Thang katika wimbo wao Tumerudi Tena (Wateule) anaposema, Ona wakali wa vina, ona tumerudi tena... msanii mwingine Juma Nature katika wimbo alioshirikishwa na Rich One unaojulikana kwa jina la Hatuna Kitu anajigamba kuwa yeye ni mkali wa vina anaposema, “...Juma Nature, Sir Nature a.k.a msitu wa vina, yeah Watanzania mahili tuliokomaa kimashairi...” Hii yote inaonesha kwa namna gani wasanii wa kizazi kipya (Hip Hop/Bongo Fleva) wanaonekana kuathiriwa na wanajadi kutokana na kuzingatia matumizi ya vina katika tungo zao na hata kujinasibisha kuwa ili uwe msanii mzuri lazima ujue namna ya kuandika na kutunga mashairi yenye vina.

Ama kwa hakika, wasanii wasanii wa Hip Hop na Bongo Fleva si kwamba wanajigamba tu kuwa wao ni wataalamu wa kutumia vina, lakini pia vina hiyo vinajidhihirisha katika tungo zao. Hebu tuangalie baadhi ya tungo kuona jinsi wasanii wanavyozingatia matumizi ya vina katika tungo zao. Tukianza na msanii Profesa Jay katika wimbo wake wa Kubwa Kuliko:
Ubeti wa 1
Yo fani ni fani muulize, Bishanga Bashaija,
Sanaa ya Bongo kwa wasanii haina faida,
Ona wenzetu Mantoni mambo safi kuku kwa mrija,
Na mimi nataka niishi kama Kadija Kadija,
Wasanii wa Bongo bado tunakufa maskini,
Nasubiri kiama changu na sijui kitafika lini,
Wazee wa serikalini semeni tatizo ni nini?
Mnataka mle jasho langu nikienda futi sita ardhini,
Hapa jasho la mtu haliliwi wala mtu haibiwi,
Jay najivinjali kama kutumia kizizi,
Machozi yananilenga nikimkumbuka mzee Nyanyusa,
Pamoja na umuhimu wake wabongo walimsusa,
Baadhi ya mafao yake wabongo wamefanya asusa,
Kwa mtu mwenye akili lazima hii itakugusa,
Tunaposema Watanzania tudumishe sanaa yetu,
Lazima mtuwekee mazingira safi ya sanaa yetu,
Marijani Rajabu tulimuita jabali la muziki,
Alifanya maajabu,alivumilia mikimikiki,
Kinachonipa ghadhabu, bwana sanaa ya Bongo hailipi,
Tofauti na chati yake, ndugu yetu amekufa na dhiki,
Sasa kipi ni kipi maana ufanisi haufanyiki,
Sababu viongozi wetu mnatamaa hauridhiki,
Wakati ni huu wa kujifunza watanzania,
Umoja wa wasanii wa bongo hiyo ndiyo njia.

Kiitikio
Ninaposema Jay kubwa kuliko,
Siko niliko ndiko liko zindiko (Yataka moyo)
Ninaposema Jay kubwa kuliko,
Siko niliko ndiko liko zindiko (Yataka moyo)
Sanaa yataka wito (yataka moyo)
Sanaa ya Bongo nzito (yataka moyo)
Sanaa ujiko mwiko (yataka moyo)
Sanaa yataka wito (yataka moyo)

Ubeti wa 2

Salamu Nicko zingilada popote roho ilipo,
Wasanii wenzako wa Bongo bado tunafanya  zindiko,
Wasalimie sana kuzimu walio hai na waliolala,
Waambie tunasuasua tu na akina Mzee Jangala,
Hardblasterz, Sikinde na Remmy Ongala,
Underground Soul  na Gangwe na Baby Stara,
Uncle Kabaino, IK pale Kimara,
OTTU Jazz na Agley Face kule Ilala,
Tunasubiri kudra za imani kwa Mungu kwa waja wake,
Tunaotafuta labda tutapata faraja zake,
Mambo si mambo yameongezeka tu matukio,
Na ajali, rushwa na UKIMWI tu ndiyo kivutio,
Sanaa imedumaa najua hiyo huwezi shangaa,
Lakini hali ya sasa ni mbaya na inatukatisha tamaa,
Soko limekuwa bovu wasanii hatuungwi mkono,
Wananchi hawana kitu kila siku wanafanya mgomo,
Kiasi wanachokipata kinaishia kwenye bia na ngono,
Na kuhusu masoko ya nje serikali imefungwa mdomo,
Mapromota wengi matapeli, ukilemaa wanakuacha feli,
Unaangua kilio, ulichotegemea kinakuwa siyo,
Wepesi kutimua mbio, wewe linakupitia fagio,
Na sasa wametuacha na kuleta wasanii wan je,
Hatimiliki ndiyo kwanza inasua sua ndani ya Bunge.

Kiitikio
Ninaposema Jay kubwa kuliko,
Siko niliko ndiko liko zindiko (Yataka moyo)
Ninaposema Jay kubwa kuliko,
Siko niliko ndiko liko zindiko (Yataka moyo)
Sanaa yataka wito (yataka moyo)
Sanaa ya Bongo nzito (yataka moyo)
Sanaa ujiko mwiko (yataka moyo)
Sanaa yataka wito (yataka moyo)

Wasanii wengi wa bongo bado tunaishi kwenye ujima,
Kiasi tunachotafuta wenye choyo wanatuzima,
Siyo lazima tupate tanuzi la kuendesha benzi au bima,
Tunachanga tuthaminiwe watanzania tupate heshima,
Nje ya mipaka, tufanye kile tunachokitaka,
Sanaa iwe ajira tuepushe wimbi la vibaka,
Heri yako Irene Ngoi milioni hazikupigi chenga,
Nakutakia kila la heri popote unapokwenda,
Si Mr. Teacher, GK wala Mzee Jongo,
Anayelidhika na maslahi ya msanii wa hapa bongo,
Yo Solo Thang, Simple X hata Onyango,
Yo Mika Mwamba, Mr Paul sina kinyongo,
Masoud Kipanya,  nathamini unachokifanya,
Oscar Makoye dodosa kusanya kusanya,
Yo African Stars, Vijana Jazz, Tatu Nane,
Sisi wote ni wasanii kwahiyo tushirikiane,
Tusaidiane kwenye pilika pilika za fani sa tuungane,
Siyo mizengwe kibao, tuwe pamoja tusitosane,
Mr 2, KU, Fid Q, TBT Crew,TQ,
Fanya mavitu kwani wakati ndiyo huu,
Soggy Doggy, Mad Brain, Eazy Braze, Hard crew,
Heyo, X Plastaz, Juma Nature na Manzese Crew,
Tuff B, Sos B, Killa B, Stieve B, Master T, Caz T,

Tukiangalia shairi hili la Profesa Jay, tunaona kuwa katika ubeti wa kwanza vina vya, a, ni,i,sa,tu, kin a ia na katika ubeti wa pili tunaona kuwa vina vya, o,la,ra,ke,a,mo,no na e wakati katika ubeti wa tatu vina vya ma,ka,nga,ngo,nya,ne na u vinajitokeza.

Vilevile tukimtumia msanii mwingine Diamond Platznum katika wimbo wake wa Kesho tunaona pia matumizi ya vina yanazingatiwa, hebu tuangalie wimbo wenyewe;
Kiitikio
Minataka kesho twende nikupeleke nyumbani
Nataka kesho twende ukamuone mama x2

Ubeti wa 1.
Kwanza kabisa ntanyonga Tai
T"shirt na Jeans ntatupa kidogo..
Unite Nasibu usiniite Dai
Asije kukuona muhuni akapandisha Mbogo...
Naukifika uagize Chai
Savanna Takila uzipe kisogo...
Kuhusu mavazi kimini haifai
Tupia pendeza ila za Hekima Logo...
 Even though wanaponda eti we ni kicheche
Waambie ndoo chaguo langu sasa wanicheke x2

Kiitikio
Minataka kesho twende nikupeleke nyumbani
Nataka kesho twende ukamuone mama x2

Ubeti wa 2.
Usilete swaga za Nainai
Ukanyoa kiduku kama Moze Iyobo..
Eti shoping twende Tai
wakati Dadaangu anaduka kigogo..
Ukikuta Nguna usikatae
we zuga unapenda hata kama wa Muhogo..
Kuhusu kabila mbona Sadai
Mama angu hana noma hata kama Mgogo
 Even though wanaponda eti we ni kicheche
Waambie ndoo chaguo langu sasa wanicheke x2

Vina vinavyojitokeza katika ubeti wa kwanza wa wimbo huu ni, ai,go na e na katika ubeti wa pili vina vinavyojitokeza ni ai,o,go na e.
Tukimtumia msanii mwingine Joh Makini katika wimbo wake wa Najiona Mimi (I see me) tunaona pia matumizi ya vina yanapewa kipaumbele kama tulivyoona kwa wasanii wengine, hebu tuangalie shairi lenyewe:

Ubeti wa 1.
Namuona Baba Mmoja Tu Juu Najiona Mimi
Namuona Mama Mmoja Tu Chini Najiona Mimi
Naziona chuki zao upendo najiona mimi
Mabegani Msalaba Wa Ndoto Mtoto Wa Mageto
Ziwe Kweli Zisiishe Kisongo Segerea Ya Keko
Juu Ya Ukweli Ndo Nifie Steven Biko
Najiona Mimi Yanapoanzia Mabadiliko
Fikra Potofu Badili Hizo
Ndoto Sio Kuzikalia Skani Mkilialia
Ndoto Ni Kuamka Mbio Kuzikimbilia
Mziki Una Hela Mwanzo Unapoingia
Hela Nyingi Zipo Mwishoni Hutozifikia For Real
Hapo Kati Kuna Kisu Siuna Jambia
Wale Papa Wabakaji Mpira Hawatotumia
Ulikuwa Mpaka Powder Utapakwa Rukaria
Na Usiambie Mtu Labda Yesu Na Maria
Baba Nikiwa Club Nakunywa Local Bia
Naomba Mziki Unaopigwa Uwe Ni Local Pia
Nyeusi Kwenye T-shirt Ndo Logo Gear
Makini Joh Na Bado Flow Ni..........Pia

Kiitikio
Ahh Internationally
I See Overtaking Wale
Najiona Mimi
Ahh I See My Sele I See Nobody Nobody Else
Najiona Mimi
Eeh Mungu Bwna Nifanyie Wepesi

I See Me International
I See Me Overtaking Wale
Najiona Mimi Eeh*2

Ubeti 2
Najiona Mimi Na Mitasi To Mary Mary
Utu Ndo Kitu Changu Ni Hery Hery
Maksi Za Show Zangu Ni A Very Very
Natia Neno Halleluya Kwenye Hali Bery
Wametuacha Mbali Na Zao Serikali Wakiunda Magari
Serikali Yangu Bando Inaunda Leseni
Ndo Maana Najiona Mimi Juu Tu Nikiunda Top Ten
Na Amka Na Hangover Ya Hela Siamki Na Deni
Na Amka Na Hangover Ya Hasira Siamki Na Demu
Nakiri Hizi Ndoto Ka Ndoto Si Grammy,BET,MTV NA Channel O
Nawakilisha Daraja Mbili Na Ngalelo
Najiona Mimi Juu Mamileo
Mawazo Juu Ya Pesa Zangu Under My Pilo
Lord Jesus My Hero Ohhh
Naona Injili Ina Shilling Siingilii Kanisani Siitilii Maanani
Sigara Saratani Siingilii Madukani
Nishida Au Umaskinii Ndo Maana Kitaa Inaua
Sugar Mamy Hajuwi Kushika Mooo
Anajuwa Kushika Mua Utashika Hela Ama Dua

Kiitikio
Ahh Internationally
I See Overtaking Wale
Najiona Mimi
Ahh I See My Sele I See Nobody Nobody Else
Najiona Mimi
Eeh Mungu Bwna Nifanyie Wepesi

I See Me International
I See Me Overtaking Wale
Najiona Mimi Eeh*2

Ubeti 3
I See Me International
I See Me Overtaking Walee
Ahh I See My Self I See Nobody Nobody Else
Napiga Goti Eeh Mungu Bwna Anifanyie Wepesi
Mwanzo Na Mwisho Si Niwe Alfa Na Omega Yes
Nalisha Neno Kwa Kila Rika Na Kila Ezi Ahhh
Mm Sio Jino Kwa Jino Nyoka Kwa Kisigino
Zima Ni Lako Neno Makini Joh uwa Simo
Ndoto Zangu Sio Zinoo
Molinge Sokoine All I Do Is Holla Up
All I Do Is Winning Najiona Kwenye Hella Mingi
Chap Chap Shule Mingi Kauli Yangu Mbiu Ni Kauli Kaa Kata Usikate Ringi

Tukiangalia shairi hili utaona kuwa msanii pia amezingatia matumizi ya vina, mathalani katika ubeti wa kwanza, vinajitokeza vina vya, mi, to,ko,zo,ia, katika ubeti wa pili vinajitokeza vina vya ri, ni,o na lo na ua, wakati katika ubeti wa tatu vinajitokeza vina vya e,si,no,mo,na ngi.
Aidha wasanii wengine, huandika mashairi yenye vina vya kati na mwisho vinavyofanana kama wanavyofanya wanajadi, Abedi (kashatajwa, uk. 5) anasema, baadhi ya watungaji (wanajadi) mwanaweka vina vya kati vya namna moja katika beti zote. Athari hii, pia tunaweza kuiona katika shairi lifuatalo kutoka kwa msanii Diamond katika wimbo wa My Nomber One;
Ubeti wa 1
Kwanza mapenzi safari, ujana ni maji ya moto
Walinenaga zamani...
Pili tumetoka mbali, matatizo changamoto
tu visa visa fulani...
tatu kidonda chako, kwangu maradhi
Mama tu usononekapo kwangu simanzi..x2
Kwa mahaba uliyonipa nimenogewa 
ni vurugu patashika punguza kidogo..
Na mengine kadharika toto si unanielewa?
Hapo hapo uliposhika...ukiongeza kidogo
mi mwenzako ntaumia

Tukiangalia ubeti huu, tutaona kuwa, katika kila kipande cha mstari cha kwanza ameweka vina vya kati vinavyolingana rejea silabi zilizokolezwa wino.

Aidha, Katika shairi hili, ubeti wa kwanza tunaona vina vya mi,to,ko na ia vimetumika wakati katika ubeti wa pili vina vya ri, ni mu, o,ni na ua hujitokeza na katika ubeti wa tatu vina vya no na ngi hujitokeza pia. Hawa ni wasanii wachache tulioamua kuwatumia kuonesha jinsi wanavyoonekana kutawaliwa na wanajadi hususani katika vipengele vya matumizi ya vina ama kwa hakika wasanii wengi wa muziki wa Hip Hop na bongo fleva wameathiliwa na utumiaji wa vina katika mashairi yao kama wanavyosisitiza wanajadi. Na wakati mwingine wasanii wa Hip Hop na Bongo Fleva huamua kutumia vifupisho ili mradi tu kuhakikisha kuwa vina vinapatikana katika tungo zao kama tunavyoweza kuona katika wimbo wa Mathematic wa Roma Mkatoliki hususani ubeti wa kwanza:
Nimeshatikisa nyavu mi ndo MVP,
Wanakimbia depo hapo nipo CCP,
Niliwapigisha kuruta kwata la JKT,
Nina kipaji mimi kushinda hata THT,
Nawapangisha foleni kama benki ya NMB,
Mi nemesoma PCM siyo PCB,
So hata tufungwe mimi ni Asernal siyo Man U,
Kibonde we ni member wa Loan Board au TCU,
Nchi imeuzwa vigogo wanatuita ATM,
Tuwakemee mafisadi wote wa CCM,
Kuvua gamba haiwasafishi mbele ya CUF,
CHADEMA mwone Makamba, JK kwa TFF,
Sihitaji dancer wala mapanga yale ya TMK,
Show zangu zangu longolongo zile za Y2K,
Na siyo bandia ka kontena lile la BOT,
Situkuzi kilicho feki kama TOT,
Mi ndio Roma ntasimama kaka KKT,
Ahsante Bongo, macho juu, Nyamongo, TBC,
Mistari yangu mitamu kama miwa ya TPC,
Na kwa hizo fomu MC utalazwa KCMC,
Kodi ya walalahoi pombe TRA,
Miili yao ndio biashara ndani ya BBA,
Fataki anatoa mikopo ndani ya TIA,
Licha ya mimba haina uhakika mpaka DNA.

Katika ubeti huu tunamuona msanii akiamua kutumia vifupisho katika kila mstari na vifupisho hivyo alivyoviteua kuvitumia vinakamilisha vina katika ubeti mzima.

Vilevile, mtindo wa wasanii kutunga na kuimba mashairi yao papo kwa papo kwa mtindo ambao wao huuita mitindo huru huku wakizangatia suala la mizani, ni ushaidi mwingine unaoonesha kuwa muziki huu unaonekana kuathiriwa na wanajadi zaidi kuliko wanausasa. Samwel na wenzake (washatajwa, uk. 63-64) wanaeleza kuwa, msanii wa Hip Hop au Bongo fleva anapotunga papo kwa papo huongozwa na fomula na hasa ile ya urari wa vina na mizani. Wanaendelea kusisitiza kuwa, fomula hii humfanya (msanii) kila mara kuhakikisha anapachika maneno ambayo yana vina. Wakimtolea mfano msanii Roma, wanatueleza kuwa katika tamasha la Epiq Nation jijini Mwanza alitoa ghani za papo kwa papo ambazo zinaonekana kuzingatia urari wa vina, kama inavyoonekana hapa chini katika ghani hizo ambap msanii ametumia vina vya ao na to ili hali mashairi hayo ameyatoa kichwani papo kwa papo;
Mwanza, msishindane na mwanamke pedeshee atamuhonga noah,
Wanaume mjitahidi ipo siku mtatoboa,
Mimi ni Rais wa ghetto,
Sina kabisa mchecheto,
Na wala sipigi punyeto,
Namiliki mademu kwa kipato,
Mwanza sema oyee kwa Epiq Nation.

Chanzo: Samwel na wenzanke (washatajwa, uk.64)

Ama kwa hakika, tukiangalia tungo za wasanii wa muziki wa Hip Hop na Bongo Fleva tutakubaliana kuwa mashairi yao kwa upande wa kuzingatia vina katika tungo zao inaelekea kuonesha kuwa wasanii wa muziki huu wanaonekana kuathiriwa sana na wanajadi.

Aidha kipengele kingine ni mizani, Abedi (keshatajwa) anafasili kuwa, mizani ni vipimo vinavyopima urefu wa kila mstari, kila silabi moja ni mizani moja. Yeye anaona shairi zuri ni lile lenye mizani16, lakini anatambua pia kuna mashairi yasiyotimiza mizani hii, hivyo anatoa maelekezo ya namna ya kuweka kina cha kati katika mashairi yenye mizani pungufu ya 16. Kupitia maelekezo haya tunaona hata wasanii wa Bongo Fleva na Hiphop wanazingatia idadi ya mizani na katika utunzi wao japo hawafuati mizani 16. Mara nyingi wamekuwa wakitumia mizani pungufu au zaidi ya 16. Mfano katika wimbo wa profesa J ametumia mizani 12. Katika wimbo wake wa kubwa kuliko hasa katika kiitikio kama inavyojionesha katika ubeti ufuatao;
   ‘ninaposema jay kubwa kuliko,
    Siko niliko ndiko liko zinduko,
    Ninaposema jay kubwa kuliko

Tukichunguza mashairi ya Hip Hop na Bongo Fleva tutaona kuwa hawazingatii ya nane nane kila kipande cha mstari ili kupata mizani 16, mara nyingi mashairi yao mizani huweza kutofautiana kati ya mstari mmoja na mstari mwingine katika ubeti mmoja lakini suala la urari wa vina huzingatiwa kama inavyojionesha katika mfano tulioutoa hapo juu, ambapo kila mstari unaishia na kina cha ko. Tukiangalia pia mfano ufuatao kutoka kwa msanii Ali Kiba katika wimbo wake wa Mwana:
Ubeti wa kwanza
Mali ni nyingi nyumbani, kipi kilichokukimbiza,
Ona babiyo mamiyo, wote wanakulilia,
Mtoto peke yako nyumbani, kipi kimekukimbiza,
Ona babiyo mamiyo, wote wanakulilia,
Ndani ya Dar Es Salaama, ulikuja bure,
Tena kimwana kimwana, hujui kuchuna,
Na zile lawama, za wallokuzoeza,
Ulikuja jana na leo tofauti sana,
Tena bora yule wa jana wa leo tofauti sana,
Dakikia mbili mbele nyuma, kichwa kinauma,
Mbona unawatesa sana,
Mbona unajitesa sana,
Ndani ya Dar Es Salaam mambo matamu hakukuhisha hamu,
We bado mtoto kwa mama hujayajua mengi,
Mwenda tezi na omo marejeo ngamani,
Amesema sana mama, dunia tambara bovu,
Kuna asali na shubiri, ujana giza na nuru,
We mwana wewe mwana, mwana jeuri sana,
Ulichokifuata hukupaa, umekosa ulivyoacha,
Kwa baba yako mwana, na mama yako mwana,
Kwa vicheche ulivyotaka, na vingi ulivyoacha,

Tukiangalia wimbo huu, tutaona kuwa mizani haijazingatiwa sana, kwani kila mstari unaweza kuwa na mizani tofauti na mstari mwingine ndani ya ubeti huo huo. Kwa mfano mstari wa kwanza una mizani 17 kipande cha kwanza cha mstari kina mizani 8 na kipande cha pili kina mizani 9, wakati mstari wa pili una mizani 16, kipande cha kwanza una mizani 8 na kipande cha pili una mizani 8. Lakini pamoja na tofauti hiyo, ya mizani, urari wa vina unazingatiwa kama inavyoonekana katika kila beti, vina vya za, a, na, cha vimetawala.

Suala lingine ambalo linasisitizwa na wanajadi ni uwepo wa kituo katika shairi. Abedi (kashatajwa uk.4) anatueleza kuwa, kituo ni mstari wa mwisho wa kila ubeti. Anaendelea kufafanua kuwa, kutuo huweza kuwa ama kiini cha habari au kimalizio. Maana hii ya kituo haipishani sana na maana inayotolewa na Wamitila (2003:93) isipokuwa anaongezea kuwa, wahakiki wengi hukiita kitua kuwa ni kibwagizo. Wasanii wa Hip Hop na Bongo Fleva hupenda kutumia istilahi ya kiitikio. Kwa wanajadi kila baada ya ubeti kama ubeti utakuwa na mistari mine basi mstari wanne ndiyo huwa kiitikio/kituo, na kwa upande wa mashairi ya Hip Hop na Bongo Fleva huwa na kituo yaani kiitikio isipokuwa wao hawana mstari maalumu ambao unapaswa kituo kiwepo isipokuwa kituo/kiitikio huwekwa mara baada ya kukamilika kwa kila ubeti. Hebu rejea mfano wa wimbo wa Profesa Jay wa Kubwa Kuliko anatumia kiitikio kifuatacho kila baada ya kukamilika kwa ubeti.
Ninaposema jay kubwa kuliko,
Siko niliko ndiko liko zinduko,
Ninaposema jay kubwa kuliko
                                                                                                                                       
Wakati mwingine kiitikio si lazima kifuate kila baada ya ubeti kwisha, wapo wasanii wengine ambao hutumia fomula ya kuanza na kiitikio kikifuatiwa na ubeti, kiitikio ubeti kiitikio, rejea mfano wa Diamond Platznum wimbo wa Kesho, msanii ameanza na kiitikio ndiyo ubeti unafuata (rejea mfano wetu wa wimbo huo tulioutoa hapo awali, pia rejea shairi la Joh Makini Najiona Mimi naye kiitikio kinajitokeza kila baada ya ubeti).

Abeid (keshatajwa) anatueleza kuwa katika mashairi ya wanajadi, kituo/kiitikio kinaweza kubadilika badilika, hali hii pia hujitokeza katika mashairi ya wanamuziki wa Hip Hop na Bongo Fleva, mfano katika shairi la wimbo wa Profesa Jay Ndiyo Mzee tunaona kiitikio cha ubeti wa kwanza kinatofautiana na kiitikio cha ubeti wa pili. Kwa mfano ubeti wa kwanza anatumia kiitikio kifuatacho;
Si mtafurahi Watanzania jamani? (ndiyo mzee)
Si ni kweli nakubalika jamani? (ndiyo mzee)
Basi mimi ni mkombozi wenu jamani (ndiyo mzee)...

Wakati katika ubeti wa mwisho anatumia kiitikio kingine na kinaimbwa na mtu mwingine (Juma Nature) anasema;
Je wananchi mmenisikia? (ndiyo mzee)
Kuwa huyu jamaa hatufai (ndiyo mzee)
Na inafaa kumchukia (ndiyo mzee)
Hatumtaki aondoke zake (ndiyo mzee)

Jambo lingine linalosisitizwa na mwanajadi katika mashairi ya kimapokeo ni kujitosheleza kwa kila ubeti. Abedi (kashatajwa,uk.4) anaona utoshelevu ni kipengele cha msingi katika shairi, anasema kuwa, kila ubeti ujitosheleze kadiri iwezekanavyo, yaani, uwe na maana kamili, na usingoje kutimizwa na ubeti mwingine. Jambo hili pia linajitokeza katika mashairi ya wasanii wa Hip Hop  na Bongo Fleva kila ubeti katika nyimbo zao huwa na maana inayojitosheleza. Ukiangalia mifano ya nyimbo tulizozitumia hapo juu ukichunguza kila ubeti utaona kuwa ubeti unajitosheleza na unatoa maana kamili. Labda kwa mfano mzuri tutumie wimbo wa msanii Jay Mo unaoitwa Story tatu Tofauti, katika wimbo huu kila ubeti umebeba kisa chake tofauti ambacho kimekamilika na unatoa maana, hebu hapa tuangalia ubeti wa tatu.
Mariam alikuwa mtoto aliyekuwa na uzuri wa peke yake,
Mi mwenyewe mmojawapo kati ya waliotaka ajiweke,
Ili anione mchumba wake,
Alisimama peke yake, alilinga kwa uzuri wake,
Tajiri familia yake, kama hanyi au hali,
Kwa jinsi alivyojisikia, na vile home kuna mali,
Kiburi alijijengea, hali iliyofanya wengi waliomjua kumchukia,
Tuliosoma naye hiyo tabia tulishaizoea,
Wazazi walisoma ndiyo maana maisha yao ya juu,
Yeye hilo hakuliona cha maana alichoona ni usister duu,
Pesa zikamtia udhaifu, za nyumbani akaona hazitoshi,
Shuleni akacheza rafu, masomo akashindwa pasi,
Alipata zero kitu ambacho wazazi hawakuamini,
Angekuwa mtoto wa kiume wangeshamfukuza nyumbani,
Wakaona siyo mbaya kama atarudia mtihani,
Kitu ambacho mariam hakikumuingia akilini,
Wakamuuliza anachotaka, akajibu computer,
Cheti akapata kwenye stashahada akachemsha,
Baada ya kupewa ujauzito, inasemekana na kizito,
Ambaye ana mke na pia nyumbani ana watoto,
Cha moto kikaanza nyumbani alipofukuzwa,
Kumbe yule kizito ana ngoma anafanya kuusambaza,
Hakumsikiliza Jose Mtambo alipoimba kizaazaa,
Yamemwaribikia mambo na mtoto bado hajazaa.

Katika ubeti huu, utaona kuwa umebeba kisa kizima kinachojitosheleza na ukisikiliza ubeti wa kwanza na wa tatu utaona kuwa kila ubeti una kisa chake kinachojitosheleza na kinachotoa maana iliyokamilika wala ahitaji ubeti mwingine ukamilishe wazo au maana ya shairi. Katika ubeti huu wa tatu msanii anaelezea tabia za Mariam, kutowasikiliza wazazi wake, kutozingatia elimu na kujikuta akipewa mimba na kuambukizwa virusi vya ukimwi.

Hitimisho.
Wasanii wa muziki wa kizazi kipya yaani Bongo Fleva na Hip Hop kama wamechota baadhi ya sifa katika ushairi wa  kimapokeo katika kutunga mashairi. Kipengele kikubwa ambacho wana-Hip Hop na Bongo Fleva wanaonekana kuathiriwa nacho ni kipengele cha matumizi ya vina katika tungo zao ambacho hasa wanajadi ndiyo wanaona kuwa ni roho ya ushairi. Lakini pamoja na hayo, pia usasa katika mashairi yao unajitokeza kwa kiasi fulani, kwa mfano yapo mashairi ya wasanii wa muziki huu ambayo hayazingatii vina lakini yanaimbika. Pia kutokuwa na idadi maalumu ya mistari katika beti za mashairi yao pia ni sifa za usasa katika utungaji wa mashairi.. Kwa ujumla hatuweza kusema wazi kuwa wanajadi ndiyo wamewaathiri wasanii wa Hip Hop na Bongo Fleva au la kwani ni jambo linalohitaji utafiti wa kina na mjadala mpana, tukiangalia hata namna muziki huu ulivyoingia nchini kwa kuiga nyimbo za wasanii wa Marekani na Ulaya ambazo nazo zinaonekana kuzingatia matumizi ya vina, vituo, kujitosheleza n.k. huenda wasanii hao ndiyo waliowaathiri zaidi. Lakini kwa mujibu wa mjadala wetu tunasema uwepo wa nduni za kijadi katika mashairi ya Hip Hop na Bongo Fleva hususani kipengele cha vina washairi hawa inaonekana na hapa tunasisitiza kuwa inaonekana kama wameathiriwa na wana jadi kwa kuwa jambo kubwa linalosisitizwa na wanajadi ni matumizi ya vina na mizani ambayo hata wana Hip Hop na Bongo Fleva nao husisitiza matumizi hayo kama tulivyoona hapo awali.




MAREJELEO
Abeid K.A. (1952) Sheria za Kutunga Mashairi na Diwani ya Amri. Ahmadiyya Printing Press.
                             Dar es salaam.

Mahenge, E (2010/2011) “Chimbuko la Muziki wa Hip Hop ni Uasi au Sanaa za Maonesho?”
                                         Katika Mulika Na. 29 & 30. TATAKI. Chuo Kikuu cha Dar es salaam.
Mbilinyi, J (Sugu) (2011) Muziki na Maisha: From the Streets to Parliament.
Mhagama, M (2008) Chimbuko la Muziki wa Kizazi Kipya Tanzania na Maana Halisi ya Neno
                                   Bongo Fleva. Imepakuliwa kutoka http://richard-mwaikenda.
                                   blogspot.com/2012/03/neno-au-jina-bongo-flavachanzo-chake.html.
                                   tarehe 11/04/2015 saa 4:15.

Mnyampala, M. (1965) Diwani ya Mnyampala.EAP. Dar es salaam.
Mulokozi, M.M na Kahigi, K.K. (1979) Kunga za Ushairi na Diwani yetu. TPH. Dar es salaam.
Mwanjoka, G. (2011) Harakati za Bongo Fleva na Mapinduzi.
Omari, S (2009) Tanzania Hip Hop as Popural Literature. Tasnifu Phd. Chuo Kikuu cha
                           Dar es Salaam.

Reuster-Jahn na Hacke (2014) “The Bongo Fleva Industry in Tanzania and Artists: Strategies
                                                   for Success.” Katika Bongo Media Words: producing and
                                                   Consuming Popular Culture in Dar Es Salaam. (Wahariri)  
                                                   Krings & Reuster-Jahn. Rudiger Keppe Verlag. Germany.

Samwel, M. (20012) Mabadiliko katika Majigambo: Uchunguzi wa Majigambo ya Jadi na ya
                                  Bongo Fleva. Tasnifu Phd. Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Samwel, M. Selemani, A.J. na Kabiero A.J. (2013)Ushairi wa Kiswahili: Nadharia, Maendeleo,  
                              Mwongozo kwa Walimu wa Kiswahili na Diwani ya Mea. Meveli Publishers.
                             Dar es salaam.     
 
Wamitila, K.W. (2003) Kamusi ya Fasihi Istilahi na Nadharia. Focus Publications Ltd. Nairobi.



Hip Hop issue  http://cdn.itvs.org/hip_hop-issue-brief-hip-hop.pdf

Mwandishi anapatikana kwa namba zifuatazo:
0715 33 55 558



No comments:

Post a Comment