Blog ya kijanja kwa ajili ya watu wajanja

Blog ya kijanja kwa ajili ya watu wajanja

Sunday, May 25, 2014

NADHARIA YA FASIHI


                                    

                                                            NADHARIA YA FASIHI

Na: Mwl. Venance F.

                                                 Fasihi ni nini?
Wapo wataalamu mbalimbali ambao wamekuwa na dhana tofauti tofauti kuhusu maana ya istilahi fasihi na wamejaribu kutoa maana mbalimbali, hivyo basi katika sehemu hii tutaangalia baadhi ya maelezo yaliyotolewa na baadhi ya wataalamu wa fasihi kufasili maana ya fasihi:

Ø  Fasihi ni kazi ya sanaa inayotumia lugha kuwasilisha ujumbe kwa hadhira au jamii iliyokusudiwa.

Ø  Tigiti Sengo na Kiango wanasema, Fasihi ni mwamvuli wa mtu na jamii na utu na maisha wa hadhi na taadhima.

Ø  Fasihi ni kielelezo cha hisia za mwandishi juu ya mambo yanayomwathiri yeye, kikundi au jamii nzima anamoishi na kwamba lengo lake kustarehesha au kufunza wasomaji wake. Fasili hii pia haikidhi maana halisi ya fasihi, je! Kielelezo hicho cha hisia za mwandishi huwasilishwa kwa kutumia nini?

Ø  Fasihi ni maandishi yanayohusu nchi au bara fulani, maandishi hayo sharti yawe ya kubuni. Ukiangalia fasili hii ina upungufu kwani fasihi si lazima yawe maandishi inaweza kuwa ni masimulizi, na si lazima yahusu nchi ama bara fulani, hivyo fasili hii inapotosha ukweli kuhusu fasihi.

Ø  Fasihi ni kazi ya sanaa inayotumia lugha kuwasilisha ujumbe au fikra za fanani.

Ø  Fasihi ni kitu chochote kilicho kwenye maandishi. Hii fasili ina mapungufu sana, kwani fasihi si lazima yawe maandishi, masimulizi pia yanaweza kuwa ni fasihi, lakini piasi chochote kilichokwenye maandishi ni fasihi kwani fasihi ni lazima kuwa matumizi ya lugha ya kisanaa.

Ø  Fasihi ni sanaa inayoakisi maisha ya jamii.

Ø  Fasihi ni chombo cha utetezi wa maslahi ya tabaka moja au jingine na kwamba mwandishi ni mtumishi wake anayejua au asiyejua, atake asitake mwandishi huyo huwa na lengo au dahamira fulani anayotaka kuionesha,wasomaji wanaweza kuikubali au kuikataa nap engine kutokana na fani, itikadi ya siasa inayotawala au jinsi mwandishi anavyoainisha.

Ø  Fasihi ni sanaa ambayo hutumia lugha teule katika kubuni tungo mbalimbali ambapo lugha hiyo teule yapaswa iwe na ufundi, mvuto wenye kusisimua ili kuwasilisha fikra zilizoko kwenye akili ya binadamu, tungo hizo zaweza kuwa hadithi, ushairi, semi, sanaa za maonesho nakadhalika.


Hivyo basi ukiangalia fasili hizo, sio zote zinazojitosheleza kutoa maana ya fasihi, ingawa fasili nyingine zinajitosheleza, lakini kwa ujumla tunaweza kusema kuwa, fasihi ni kazi ya sanaa unayotumia lugha mahususi yenye mvuto, mguso wa kusisimua ili kuwasilisha ujumbe, fikra au mawazo ya fanani kwa hadhira aliyoikusudia, fikra au mawazo hayo sharti yawe ya kubuni.

Sanaa imefasiliwa kuwa ni kazi ya mikono na/au akili ya mtu, nayo aghalabu ina umbo dhahiri lenye maana kamili.[Mbunda M.:1992]

Sanaa pia, imefasiliwa kuwa ni uzuri unaojitokeza katika umbo lililosanifiwa, umbo ambalo mtu hutumia katika kuelezaea hisi zinazomgusa au kutoa kielelezo chenye maana maalumu.

Tazama kielelezo Na. 1: Mchoro wa Sanaa na Matawi yake.

     SANAA
USUKAJI
MUZIKI
UWINDAJI
MAONESHO
UWINDAJI
USUSI
FASIHI
UFINYANZI
UTARIZIiiI
UCHONGAJI
 













                                                            
                                                     Mwanzo wa Fasihi
Wanafasihi mbalimbali wa ndani na nje wametoa mawazo yao kuhusu chimbuko/mwanzo wa fasihi, kutokana na mawazo hayo ya wanafasihi kuhusu mwanzo wa fasihi, tunapata mitazamo/nadharia ya namna mbili {2} ambayo ni:

                                                 [i] Mtazamo wa Kidhanifu
                                                 [ii] Mtazamo wa Kiyakinifu

Labda swali la kujiuliza, kwanini, mitazamo hiyo inaitwa, mtazamo wa kidhanifu na kiyakinifu? Jibu ni kwamba watetezi wa mitazamo hiyo hutumia hoja mbalimbali kuthibitisha chanzo au mwanzo wa fasihi, wapo wanaotumia hoja ambazo ni vigumu kuthibika na hivyo kuwa ni hoja zinazotokana na dhana ya kufikirika na ndio maana tunasema mtazamo wa kidhanifu maana hoja zao huwa ni dhana tu. Wakati pia wapo wanaotumia hoja ambazo zinathibitika kisayansi na ndio maana tunasema kuwa ni mtazamo wa kiyakinifu, hivyo basi katika sehemu hii tutajadili mitazamo hiyo kulingana na wataalamu mbalimbali wa fasihi, tukianza na:

[i] Mtazamo wa Kidhanifu
Kama tulivyoweza kuona hapo juu, watetezi wa mtazamo huu, hutoa hoja ambazo ni vigumu kuthibika kisayansi na hivyo kuonekana kama ni dhana tu za kufikirika na ndio maana ukaitwa mtazamo wa kidhanifu. Huu ni mtazamo mkongwe sana kwani ulikuwepo hata kabla ya kuzaliwa Kristo Watetezi wa mtazamo huu wanasema kuwa, fasihi ni zao au kazi ya Mungu na binadamu huiga kazi hiyo kutoka kwa Mungu ambaye ndiye chanzo cha sanaa zote duniani, watetezi wa mtazamo huu wanaamini kuwa sanaa na fasihi kwa ujumla zilitoka kwa Mungu na mwandamu huipokea sanaa hiyo ikiwa imepikwa na kuivishwa na Mungu na hadhira huipokea sanaa/fasihi hiyo ikiwa imechujuka mara tatu [3] yaani inatoka kwa Mungu, inamfikia fanani na fanani huiwasilisha kwa hadhira.

Tazama kielelezo Na. 2 

MUNGU
  MSANII
HADHIRAHIRA HADHIRA
       
                                          


Wayunani na Wagiriki wa kale huko Ulaya walikuwa na miungu ya ushairi na muziki waliowaita Muse ambao walikuwa wakiwaamini kuwa ndio waliokuwa wakiwapa wasanii/watunzi msukumo wa kiroho, kinafsi na kijazba wa kutunga kazi za fasihi, watetezi wa mtazamo huu wanaamini kuwa Mungu ndiye msanii mkuu na na hivyo uwezo wa binadamu kubuni kapewa na Mungu.
      
Mfano wa watetezi wa mtazo huu ni pamoja na Socrates, Plato na Alistotle, hawa ni wanafalsafa wa mwanzo kabisa wa Kigiriki na Kirumi ambao wanaamini kuwa chanzo cha sanaa na fasihi ni Mungu na humfikia mtumiaji ikiwa imechujuka mara tatu kama tulivyoona hapo juu.

Kwa upande wa wataalamu wa fasihi ya kiswahili pia wapo baadhi ya wataalamu wanaokubaliana na akina Plato kuwa chanzo cha sanaa na fasihi ni Mungu, na mfano wa wataalamu hao ni kama vile; F. Nkwera na John Ramadhani, mathalani F.Nkwera katika kuunga mkono mtazamo huu anasema, “…fasihi ni sanaa ambayo huanzia kwa Muumba na hunfikia mtu katika vipengele mbalimbali…” anaendelea kusema kuwa, “Fasihi ni hekima ambayo mtu ameshirikishwa apate kumtambua Muumba wake.”
Hapa anachotuambia Nkwera ni kuwa fasihi huanzia kwa Mungu hivyo chanzo cha fasihi kwa mujibu wa maelezo yake ni Mungu.

Naye John Ramadhani anasisitiza kwa kusema kuwa, “.Zaidi ya kwamba fasihi ni hisi, vilevile kitendo cha mtu cha kubuni kazi ya sanaa ni uigaji wa Mungu ambaye ndiye mfalme wa sanaa zote.”

Vilevile wapo wataalamu wengine wanaounga mkono mtazamo huu, wanaamini kuwa matengenezo ya sanaa huonekana kama kazi ya kiungu yenye kumuiga Mungu ambaye wanaamini kuwa ndiye Msanii wa kwanza kabisa.

Kiufupi F.Nkwera na John Ramadhani wanaami kuwa Mungu ndiye muumba wa fasihi, fasihi hutoka kwa Mungu na kumfikia mtu kwa njia mbalimbali na njia ya mwisho ni darasani.

Hivyo basi ukiangalia hoja zinazotolewa na watetezi wa nadharia hii ni za kidhanifu mno, ni hoja ambazo za kufikirika tu na ambazo haziwezi kuthibitishwa kisayansi kama ni kweli au la! Ni hoja zenye udhaifu mkubwa zinazochanganya taaluma na imani.

Udhaifu wa Mtazamo huu
Ø  Wtaalamu wote wa fasihi wanakubaliana kuwa fasihi ni mwigo, sasa kama fasihi ni mwigo kama fasihi ni huigwa kutoka kwa Mungu, je! Mungu yeye huiga kutoka kwa nani?
Ø  Mungu ni mwenye upendo, na kama Mungu ni mwenye upendo kwanini wengine awapendelee wengine kwa kuwapa hekima ili wapate kumtambua yeye?
Ø  Huu ni mtazamo wa kibinafsi kwani humuweka msanii au fanani kuwa karibu sana na Mungu kuliko watu wengine
Ø  Mtazamo huu pia hukuza hali ya utabaka kati ya msanii/fanani na hadhira yake kwa kujiona kuwa yeye ni bora sana kuliko hadhira yake kwa kuwa amepewa hekima na Mungu.
Ø  Nadharia hii inachanganya taaluma na imani zaidi jambo ambalo halikubariki kabisa katika taaluma na hivyo kuonekana kuwa hoja za mtazamo huu kutokuwa na mashiko zaidi.

Mtazamo wa Kiyakinifu
Fasihi ni sanaa ya lugha. Je! Kama fasihi ni sanaa ya lugha, lugha ilianzaje?
Wanasayansi wenye mtazamo wa kiyakinifu wanaona kuwa chimbuko la lugha linatokana na utumiaji wa dhana za kazi, wanaeleza kuwa, viumbe yaani sokwe walipoanza kubadilika na kuwa watu wakaanza kuwa viumbe wenye hisi, walitoa milio ya uchungu, ya furaha, hasira, tahadhari pamoja na kuonesha hisi hizo walikuwa wanaonesha ishara zao kwa kutumia viungo vyao vya mwili.

Viumbe hawa baada ya kushuka chini na kuanza kusimama wima kwa miguu miwili walianza kutengeneza na kutumia zana kwa mikono yao kwa kushirikiana [kumbuka haya yalikuwa ni mambo ya taratibu na yalichukua muda] kwa maana hiyo ili shughuli za kazi za kijima ziweze kufanikiwa palihitajika chombo cha mawasiliano thabiti, hivyo basi baada ya muda kupita binadamu akaanza kusema na maneno hayo yalikuwa yakiiga sauti za zana katika kufanya kazi {mwigo wa zana za kazi}

Hivyo basi lugha ilizuka katika mazingira hayo ya shuguli za kufanya kazi, na kwa kuwa lugha ni chombo muhimu cha fasihi na ndivyo fasihi ilivyozuka kwa namna hiyo na ushaiti ndiyo fasihi ya mwanzo kabisa.

Hivyo basi kutokana na ushahidi huo, watetezi wa nadharia hii hudai kuwa “Binadamu ndiye alfa na omega wa fasihi”

Baadhi ya wataalamu wa fasihi ambao kwa namna moja ama nyingine hukubaliana na mawazo hayo kuwa binadamu ndiye chanzo cha fasihi, ni kama vile:


1.      Richard, yeye anasema kuwa, Sanaa [ushairi/fasihi] inatokana na mambo makuu manne [4] ambayo ni;
                               {i} Upweke wa binadamu
                               {ii} Ujinga wa binadamu
                               {iii} Nafasi ya binadamu katika upana na wakati
                               {iv} Ukweli kuhusu kifo na kuzaliwa

Hii ina maana kuwa, upweke wa binadamu ulimfanya aanze kutafuta kitu kitakachomuondolea upweke katika mazingira aliyokuwa akiishi na hapo ndipo fasihi ikaziliwa ili kuwa chombo cha kumburudisha binadamu na kumuondolea upweke. Na ujinga wa binadamu unatokana na kuwa kipindi hicho cha ujima hakukuwa na maendeleo ya sayansi na teknolojia yaani zilikuwa zama za ujinga, kwa maana hiyo zana za kufanyia kazi kipindi hiko zilizobuniwa na binadamu zilikuwa duni mno na hivyo kuanza kutafuta nyenzo itakayomsaidia binadamu kufanya kazi na kuzalisha zaidi na hapo ndipo fasihi ikazaliwa ili kumchochea binadamu kufanya kazi na ndio maana inasemekana kuwa wimbo wa kazi ndio fasihi ya mwanzo kabisa. Pamoja na nafasi ya binadamu katika upana na wakati na ukweli kuhusu kifo na kuzaliwa ndizo shughuli zilizomfikirisha binadamu mpaka akabuni sanaa/fasihi.

2.      Senkoro F.M naye katika kitabu chake cha Fasihi na Jamii katika kuunga mkono mtazamo huu, anasema, binadamu ndiye alfa na omega wa fasihi, na anaendelea kusema kuwa, katika kipindi cha ujima, binadamu alianza kutumia zana kama mawe na mifupa kutumia kama silaha na kufanyia kazi, hisia za kisanaa zilianza kutumika katika kutekeleza kazi kwa nyenzo bora zaidi, wimbo wa kazi ndiyo fasihi ya mwanzo kabisa na ushairi wa mwanzo ulifungamana na nyimbo na ulitungwa kwa kufuata mapigo ya zana za kazi, chanzo cha sanaa ni kazi.

3.      Kezilahabi E. naye anasema, kila binadamu ana uwezo wa kuumba fasihi. Katika kuipa uzito hoja yake, Kezilahabi anatoa mfano wa motto anapozaliwa na kulia kuwa hiyo ndiyo dalili ya fasihi yake ya mwanzo kabisa, yaani shairi lake la kwanza kutunga.

Hizo ndiyo hoja ambazo, wataalamu wengi wa fasihi wanakubaliana nazo kuwa chanzo cha fasihi ni binadamu mwenyewe kuonekana kuwa na mashiko zaidi kuliko ule mtazamo wa kidhanifu  .

Dhima za mtunzi wa kazi za fasihi
  1. Mtunzi wa kazi za fasihi ana dhima ya kuelimisha jamii yake, hii inatokana na ukweli kuwa, katika kazi za fasihi huwa na maudhui mbalimbali ambayo kwayo hadhira huweza kuelimika. Mathalani katika wimbo wa starehe uliotungwa na kuimbwa na msanii Ferouz unaielimisha jamii kuhusiana na ngono zembe kuwa mwisho wake ni kuambukizwa virusi vya ukimwi, na katika riyaya ya Pesa zako Zinanuka iliyoandikwa na Ben Mtobwa anaielimisha jamii juu ya athari ya ufisadi na uhujumu uchumi. Pia zipo kazi nyingine za watunzi wa kazi za fasihi zinazoelimisha juu ya matumizi sahihi ya vyandarua, umuhimu wa kupiga kura n.k

  1. Mtunzi wa kazi za fasihi pia ana dhima ya kuiburudisha jamii yake, hii ina maana kuwa jamii inapokuwa imechoka kutokana na shughuli za uzalishaji mali uhitaji kupumzika na hivyo kazi ya mtunzi wa kazi za fasihi ni kuiburudisha jamii yake, mfano kupitia nyimbo mbalimbali, vichekesho, mathalani vichekesho vinacyooneshwa katika luninga kama vile TBC {Original Comedy}, EATV {The Comedy} na Star tv {Futuhi} huwa na dhima kubwa ya kuiburudisha jamii kwa kiasi kikubwa kwa njia ya kuchekesha lakini wakati huo huo wakitoa elimu.

  1. Dhima nyingine ya mtunzi wa kazi za fasihi ni kuikosoa jamii yake pindi anapogundua kuna maovu yanafanyika katika jamii yake, kwa mfano msanii Mrisho Mpoto kupitia kazi zake amekuwa akiikosoa serikali na jamii kwa ujumla, rejea nyimbo zake za Nikipata Nauli, Asanteni kwa kuja na Adera ambapo katika wimbo wa Nikipata nauli anakosoa urasimu uliopo serikalini, ufisadi na kukumbatia viongozi wasiowaadirifu. Vilevile mwandishi E. Kezilahabi katika tamthiliya yake ya Kaptura la Marx anaikosoa serikali na jamii yake kwa ujumla kukumbatia sera za kigeni pasina kuzifanyia utafiti na matokeo yake kushindwa kuendelea mbele.

  1. Kutia hamasa au kuhamasisha jamii, ni dhima nyingine ya mtunzi wa kazi za fasihi, mtunzi ana dhima ya kuihamasisha jamii kuacha au kufanya jambo fulani kupitia kazi zao, mathalani katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 vikundi mbalimbali vya sanaa vilitunga nyimbo zenye lengo la kuhamasisha jamii kukichagua chama fulani na mgombe wake. Kwa mfano kulikuwa na wimbo unaoitwa Anaweza Dr.Slaa uliokuwa ukiwahamasisha wananchi kumchagua Dr. Wilbroad Slaa kuwa Rais lakini pia kulikuwa na wimbo wa Anafaa ulioimbwa na TMK Family uliokuwa ukiwahamasisha wananchi kumchagua Dr. Jakaya Mrisho Kikwete.

  1. Dhima nyingine ya mtunzi wa kazi za fasihi ni kuionya jamii yake. Kwa mfano msanii 20% katika wimbo wake wa Tamaa mbaya, anaionya jamii yake kuchunga tamaa kwani ni mbaya, lakini pia msanii Profesa J katika wimbo wake wa Bongo Dar es salaam anaionya jamii yake kuwa makini na mji wa Dar-es-salaam kwani umejaa kila aina ya utapeli.

  1. Mtunzi wa kazi zafasihi ana dhima ya kueleza na kuikumbusha jamii historia ya jamii. Mtunzi wa kazi za fasihi wakati mwingine anakuwa na dhima ya kuelezea na kuikumbusha jamii yake ni wapi imetoka, kwa mfano tamthiliya ya Mkwava wa Uhehe kilichoandikwa na M.M. Mulokozi mtunzi anaelezea historia ya Chifu Mkwawa wa Wahehe na mapambano yao dhidi ya uvamizi wa Wajerumani, pia kuna kitabu cha Kinjeketile kilichoandikwa na Hussein kinachoelezea vita vya maji maji.

  1. Mtunzi wa kazi za kifasihi pia ana dhima ya kukuza lugha, hii ina maana kuwa msanii anapoamua kuteua lugha ili kuweza kuwasilisha mawazo au ujumbe wake kwa hadhira hujikuta akiibua msamiati mpya ambao huweza kutumika kama misimu na pindi inapopata mashiko kimatumizi husanifishwa na kuwa msamiati sanifu na hivyo kuchangia lugha kukua kimsamiati, lakini pia kazi zao kusomwa au kusikilizwa na watu wengi pia huchangia lugha kusambaa na kuenea sehemu mbalimbali na kuvuka mipaka kimatumizi.
                                 
Mawasiliano: 0715 33 55 58 (whatsapp)
                       0755 44 06 99
Nifollow instagram: fullraha17
Facebook: Furaha Venance

Sunday, May 18, 2014

MKONO ATUHUMIWA KUWAHONGA WABUNGE KUKWAMISHA BAJETI YA WIZARA YA NISHATI NA MADINI, MWENYEWE AMWACHIA SPIKA.


Dodoma. Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (Pichani kushoto) na Mbunge wa Musoma Vijijini, Nimrod Mkono wameingia katika mvutano baada ya ujumbe wa maandishi wa kutaka kukwamisha bajeti ya wizara hiyo kusambazwa kwa wabunge.
Habari za uhakika zilizopatikana jana zilieleza kuwa kiini cha mgogoro huo ni ujumbe mfupi (SMS) ambao unamtuhumu Mkono kula njama za kutaka kukwamisha bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini.
Gazeti hili limedokezwa kuwa, SMS hiyo inadaiwa kutumwa na Waziri Muhongo kwenda kwa baadhi ya wabunge akimtuhumu Mkono kuwahonga baadhi ya wabunge Sh3 milioni kila mmoja ili kukwamisha bajeti hiyo.
Ujumbe huo unasomeka ”Mhe Spika wa Bunge la Jamhuri, Sisi wabunge waadilifu tunakiri kwamba Mhe Mkono ametufuata na kutupatia fedha kila mmoja milioni 3 ili tukwamishe bajeti ya Nishati na Madini.
Ujumbe huo umeanza pia kusambaa kwenye mitandao ya kijamii ikiwamo Jamii Forums .
Mkono
Mkono ambaye pia ni Mwanasheria mashuhuri nchini, alipoulizwa jana kama ni kweli amelalamika kwa Spika juu ya jambo hilo, alikiri na kusema alichofanya ni kulalamika kwa Spika na amemwachia alishughulikie.
“Ni kweli nimelalamika kwa Spika. Unajua taratibu za Bunge ni kuna any complaint (lalamiko) unaliwasilisha officially (rasmi) kwa Spika… hilo jambo lipo nimelifikisha kwa Spika wao ndiyo watafuatilia kwa taratibu zao,”alisema.
Profesa Muhongo
Alipotafutwa kwa njia ya simu ili alitolee ufafanuzi suala hilo, Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo alituma ujumbe kwa simu ukisema:
“Tutavuka tukiwa na ushindi wa maskini na wanyonge wa nchini mwetu. Tutaendelea kujenga uchumi imara utakaotoa ajira mpya na matumaini mapya kwa vijana, maskini na wanyonge wa nchini mwetu. Watanzania wamechoshwa na wizi, udalali, ubabaishaji na rushwa.”
Mkurugenzi wa shughuli za Bunge, John Joel alipotafutwa jana alisema yeye hana taarifa juu ya jambo hilo akisema kama lipo, basi huenda likawa mikononi mwa Spika mwenyewe.

Mvutano huo unakuja siku chache baada ya Sakata la IPTL lililoibuliwa Bungeni Ijumaa iliyopita na mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila ambaye alisema kuna ufisadi wa zaidi ya Sh200 bilioni katika akaunti ya Escrow iliyopo chini ya Benki kuu ya Tanzania (BoT).
Akaunti hiyo ilikuwa ni ya pamoja kati ya IPTL na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kuhifadhi malipo ya kila mwezi kwa IPTL katika kipindi chote cha mgogoro kati IPTL na Tanesco ambao uliishia mahakamani.
Tayari Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limemwagiza Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kuchunguza sakata hilo.
Alhamisi wiki hii, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema aliliambia Bunge kuwa wapo watu wanaonunua mashahidi kuhusiana na sakata hilo ingawa hata hivyo hakuwataja kwa majina.

MWANANCHI

Wednesday, May 14, 2014

MTATIRO AMPA MAKAVU KITILA MKUMBO, ADAI, UKAWA HAINA NIA YA KUVUNJA MUUNGANO



Mwalimu Kitila Mkumbo, UKAWA inapigania na kutetea misingi mikuu ya maoni ya wananchi iliyomo katika rasimu ya katiba. Kabla hatujaenda bungeni hakukuwa na UKAWA, UKAWA ilikuja haraka sana baada ya kuona mbinu chafu za CCM kuzuia maoni halali ya wananchi. Mtikila tunafanya naye kazi kwa sababu pia ameunga mkono kutetea maoni ya wananchi. Kwa kweli kinachotuunganisha sote hivi ss ni kutetea maoni ya wananchi.

Hoja ya nia ya UKAWA kuvunja muungano si kweli, nimeshasema hapo juu kuwa tunataka maoni ya wananchi yaheshimiwa, na wananchi walisema muungano lazima uwepo, wakasema uwe wa serikali tatu. Thats all. Ajenda yetu kuu kwa sasa n kutetea mamlaka, matakwa na maoni ya wananchi. Katika kushirikiana kuwatetea wananchi mambo kadhaa yamejitokeza na nitayataja.

Kwa mara ya kwanza katika historia ya demokrasia ya vyama vingi Tanzania, viongozi wakuu wa vyama ambao kuna wakati walijiona kama maadui wamepata fursa ya kufanya kazi kwa karibu sana na pamoja, wamejenga njia ya kuanza kuaminiana na kujihakikishia kumbe wanaweza kufanya kazi pamoja. Na hili kwangu mimi ni jambo jema sana. Leo Lipumba, Mbowe, Mbatia na wengine wanaalikaba hadi majumbani na kujadili mwelekeo wa nchi yetu, leo viongozi wamekuwa karibu sana. Mimi naliona kama jambo la heri mno.

Pia, viongozi wameendelea na nia ya kushirikiana katika masuala ya bunge(limefanyika) na wana mipango vyama vishirikiane baadaye hata katika masuala ya uchaguzi(HILI PIA NI TAKWA LA WANANCHI). Mie kama kijana naona siku za usoni panaweza kuwa na ushindani mkubwa zaidi wa kisiasa ikiwa vyama na wadau muhimu watafanya kazi pamoja.

Tuachane na huko, turudi kwenye suala la UKAWA kutaka kuvunja muungano.
Mwalimu wangu, hivi majuzi wewe na wenzio wachache mlikuwa mkipigania mabadiliko makubwa ya kidemokrasia ndani ya CHADEMA, na mlidhani kuwa wanaCHADEMA wengi wangetaka mabadiliko ikiwa yatafanywa kidemokrasia ndani ya chama chao. Je kwa akili za harakaharaka na nyie mlikuwa na lengo la KUIUA na KUIVUNJAVUNJA Chadema? Ikiwa unaamini kuwa UKAWA kupigania maoni ya wananchi yaheshimiwe ni kuvunja muungano, Je unaamini pia wewe na Zitto Kabwe kupigania demokrasia ndani ya CHADEMA ilikuwa ni KUIVUNJA Chadema? Tusipotoshe umma katika masuala ambayo yako wazi. Ndiyo maana mlipotofautiana ndani ya CHADEMA sisi wengine tulijua mna madai ya msingi mno. Hatukutoka hadharani kuja kuwashutumu eti madai yenu ni kuivunja Chadema, japokuwa viongozi mbalimbali wa CHADEMA walisema hadharani kuwa mlikuwa na nia ya kuisambaratisha(SHUTUMA HIZI MLIZOPEWA MIMI SIZIAMINI HATA KIDOGO).

Umemtaja Tundulisu, nakubaliana nawe sana. Kuna wakati aliwahi kuwaponda sana wazanzibari, kuna wakati aliwahi kuwa na ajenda ambayo huwezi kuifahamu, alifanya mambo ya ajabu mno. Wakati ule ulikaa kimya, Hukumkosoa kwa sababu ambazo sizijui, leo wakati mnatofautina kiitikadi unamkosoa.
Nataka tu kusema kwamba, pamoja na madhaifu na mapungufu ya mmoja mmoja kati yetu, pamoja na madhaifu yanayoweza kuwepo katika kundi zima, pamoja na hofu nyingi za watawala juu ya UKAWA. Bado UKAWA haitatoka katika msitari wa ajenda yake. Wananchi waliona tulivyowasilisha maoni ya wachache, wanajua kila tulichosema.

Tunaamini katika muungano wa haki, muungano wa kidemokrasia, muungano uliopendekezwa na wananchi au vyombo vyenye mamlaka kama zilivyowahi kufanya tume za Nyalali, Kisanga, G55, Warioba n.k. Tunaamini kuwa serikali ya Tanganyika ikirudi muungano utakuwa imara zaidi, kama umedumu kwa miaka 50 Zanzibar ikiwepo, hautashindwa kudumu miaka mingine 50 Tanganyika nayo ikiwepo.
Hizi hofu za muungano kuvunjika hazitusaidii. Muungano unahitaji nia ya dhati ya viongozi na hasa utashi wa kuuendeleza, tutumie fursa hii kuwasikiliza wananchi. Sisi hatutarudi nyuma, tutasonga mbele kuhakikisha maoni ya wananchi yanaheshimiwa.

J. Mtatiro