Blog ya kijanja kwa ajili ya watu wajanja

Blog ya kijanja kwa ajili ya watu wajanja

Sunday, May 18, 2014

MKONO ATUHUMIWA KUWAHONGA WABUNGE KUKWAMISHA BAJETI YA WIZARA YA NISHATI NA MADINI, MWENYEWE AMWACHIA SPIKA.


Dodoma. Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (Pichani kushoto) na Mbunge wa Musoma Vijijini, Nimrod Mkono wameingia katika mvutano baada ya ujumbe wa maandishi wa kutaka kukwamisha bajeti ya wizara hiyo kusambazwa kwa wabunge.
Habari za uhakika zilizopatikana jana zilieleza kuwa kiini cha mgogoro huo ni ujumbe mfupi (SMS) ambao unamtuhumu Mkono kula njama za kutaka kukwamisha bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini.
Gazeti hili limedokezwa kuwa, SMS hiyo inadaiwa kutumwa na Waziri Muhongo kwenda kwa baadhi ya wabunge akimtuhumu Mkono kuwahonga baadhi ya wabunge Sh3 milioni kila mmoja ili kukwamisha bajeti hiyo.
Ujumbe huo unasomeka ”Mhe Spika wa Bunge la Jamhuri, Sisi wabunge waadilifu tunakiri kwamba Mhe Mkono ametufuata na kutupatia fedha kila mmoja milioni 3 ili tukwamishe bajeti ya Nishati na Madini.
Ujumbe huo umeanza pia kusambaa kwenye mitandao ya kijamii ikiwamo Jamii Forums .
Mkono
Mkono ambaye pia ni Mwanasheria mashuhuri nchini, alipoulizwa jana kama ni kweli amelalamika kwa Spika juu ya jambo hilo, alikiri na kusema alichofanya ni kulalamika kwa Spika na amemwachia alishughulikie.
“Ni kweli nimelalamika kwa Spika. Unajua taratibu za Bunge ni kuna any complaint (lalamiko) unaliwasilisha officially (rasmi) kwa Spika… hilo jambo lipo nimelifikisha kwa Spika wao ndiyo watafuatilia kwa taratibu zao,”alisema.
Profesa Muhongo
Alipotafutwa kwa njia ya simu ili alitolee ufafanuzi suala hilo, Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo alituma ujumbe kwa simu ukisema:
“Tutavuka tukiwa na ushindi wa maskini na wanyonge wa nchini mwetu. Tutaendelea kujenga uchumi imara utakaotoa ajira mpya na matumaini mapya kwa vijana, maskini na wanyonge wa nchini mwetu. Watanzania wamechoshwa na wizi, udalali, ubabaishaji na rushwa.”
Mkurugenzi wa shughuli za Bunge, John Joel alipotafutwa jana alisema yeye hana taarifa juu ya jambo hilo akisema kama lipo, basi huenda likawa mikononi mwa Spika mwenyewe.

Mvutano huo unakuja siku chache baada ya Sakata la IPTL lililoibuliwa Bungeni Ijumaa iliyopita na mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila ambaye alisema kuna ufisadi wa zaidi ya Sh200 bilioni katika akaunti ya Escrow iliyopo chini ya Benki kuu ya Tanzania (BoT).
Akaunti hiyo ilikuwa ni ya pamoja kati ya IPTL na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kuhifadhi malipo ya kila mwezi kwa IPTL katika kipindi chote cha mgogoro kati IPTL na Tanesco ambao uliishia mahakamani.
Tayari Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limemwagiza Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kuchunguza sakata hilo.
Alhamisi wiki hii, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema aliliambia Bunge kuwa wapo watu wanaonunua mashahidi kuhusiana na sakata hilo ingawa hata hivyo hakuwataja kwa majina.

MWANANCHI

No comments:

Post a Comment