Blog ya kijanja kwa ajili ya watu wajanja

Blog ya kijanja kwa ajili ya watu wajanja

Saturday, August 31, 2013

FAHAMU HISTORIA YA WAIRAQW NA ASILI YA JINA MBULU

Wairaqw ni moja ya makabila matatu tu Tanzania ambalo ni jamii ya Wakushi au Wahamitiki wenye asili yao kwenye nchi za Ethiopia tofauti na wengi wanavyoamini kuwa asili yao ni mesopotamia yaani Iraq ya sasa(mengine ni Wambugu waliopo Tanga na Wagorowa au wafyomi waliopo Babati). Utafiti wa kiathropolojia na hata vinasaba (DNA) uliofanyika unathibitisha kuna uhusiano mkubwa kati ya Wairaqw na hao wakushi wa Ethipia na Eritrea, kuanzia muundo na matamshi ya lugha, miili (body structure), mavazi na hata shughuli za kila siku ikiwemo hata michezo kwani Wairaqw kama walivyo waethipia wanasifika kwa riadha na wamefanana katika kila hali
 

 
Kutokana na sababu ambazo hazifahamiki japo inaaminika kuwa ni kwa sababu ya vita au njaa ya mara kwa mara inayoikumba eneo hilo la pembe ya Afrika, kundi moja la watu lilihama kuelekea kusini kufuata bonde la ufa kwa miaka mingi sana. Walipofika kaskazini kwa Tanzania ya sasa, wakagawanyika makundi mawili ambapo kundi moja dogo lilielekea mashariki na kundi lingine likaendelea na safari yao wakifuata bonde la ufa kuelekea kusini. Kundi hilo dogo lilifika mpaka milima ya usambara Tanga na kukaa huko mpaka leo ambao ndio wanaofahamika kama Wambugu.

 
Inasemekana kundi kubwa liliendelea kusonga mpaka kusini mwa Tanzania hadi Iringa wakaishi huko kwa miongo mingi sana kabla ya kuamua kurudi kaskazini baada ya kuona eneo hilo haliwatoshi baada ya kustawi sana hapo. Katika thesis yake ya PHD, Dr. Jackson Makwetta ambaye ni Mhehe aliandika kuwa jina la wahehe limetokana na kabila moja dogo ambalo liliishi zamani karibu na wahehe ambalo kwa sasa lipo wilayani Mbulu mkoani Arusha (sasa Manyara) ambalo wao kila wakimwona mtu asiye wa kabila lao walimwita Hee! Hee! 

 
Lakini pia, masimulizi ya wazee wa kiiraqw yanaanzia kwenye sehemu inayoitwa Gusir Ma/angwatay, nchi inayoelezwa kuwa ni ya baridi sana iliyopo kusini, ambapo hawakumbuki wala hakuna masimulizi yanayoeleza kabla ya kufika hapo walitoka wapi lakini wanajua baada ya kuondoka hapo wakafika sehemu inayoitwa Gusir Tiwalay yaani sehemu tuliyopigwa. Hapa ndipo historia ya Wairaqw ilipoandikwa upya na kuchukua sura nyingine kabisa, eneo hili inasemekana ni kati ya Babati, Hanang na Kondoa.
 
Wakiwa hapa, wairaqw walistawi sana wakiwa na ng`ombe na mazao ya kutosha, wakashamiri katika michezo na mafunzo ya kivita lakini hawakuwa na watu wa kupigana nao. Masimulizi yanaeleza kuwa katika kipindi hiki mchezo wa kupigana kwa fimbo yaani Ilgendi ulishamiri sana ambako kulikuwa na hadi mashindano ya kutafuta bingwa wa mchezo huo. Vijana wakajawa na kiburi na kuona wao ni wao, wakamshinikiza kiongozi wao aliyeitwa Haymu Tippe awaletee watu wa kucheza nao (kupigana nao) na kumteka mtoto pekee wa Haymu na kumtishia kuwa kama hatawaleta watu wa kupigana nao watamuua huyo mtoto. Japo Haymu Tippe aliwaasa hasa baada ya ramli yake kuonesha madhara makubwa yatakayotokana na vita hivyo lakini vijana hao waliushikilia msimamo wao, walidai vita.
 
Haymu akaenda akawafuata wadatoga lakini kabla hawajafika, Haymu alitoroka na baadhi tu ya watu wa ukoo wake (Tippe) na ukoo wa Duwe na Naman (wengine wanadai ni Masaay) ambao ndio waliomsikiliza. Waliobaki nyuma na kusubiri vita walimalizwa wote na hakubaki hata mtu moja. Katika kukimbia huko, Haymu alikuwa na mpwa wake (mtoto wa dada yake) aliyeitwa Gortoo ambapo katika kukimbia kuelekea ukingo wa bonde la ufa kwa kaskazini waligawanyika huku Gortoo akiwangoza kundi dogo kuelekea mlima Kwaraa uliopo Babati na Haymu Tippe na kundi lingine wakielekea mlima Hanang (/Anang) lakini wakaamua kukimbilia kwenye kingo za bonde la ufa eneo la Madunga na kisha kufuata kingo hizo kuelekea Kaskazini Mashariki hadi milima ya Tlahhara na Nou hadi Irqwar Daaw sehemu inayoitwa Mama Isara.
 
Gortoo na kundi lake wakakaa huko Kwaraa na maeneo ya Babati na ndio wakawa kabila la Gorowa au Wafyomi ambao kwa sehemu kubwa wamefanana na wairaqw isipokuwa baadhi ya matamshi ya maneno kutokana labda na mabadiliko ya mazingira lakini wanasikilizana.
 
Wairaqw waliishi hapo Mama Isara kwa miaka mingi sana na kuanza kuongezeka kutoka hizo koo tatu tu, wakaanza kupokea watu kutoka koo mbalimbali (assimilation) na kuunda koo mpya, mfano ukoo wa Bayo uliundwa na Wanyiramba waliofikia kwa mtu anayeitwa Bayo na kisha kuitwa Manda do Bayo! Aidha ukoo mkubwa kuliko wote wa Wairaqw ambao ni Sulle asili yao ni Wadatoga na utafiti unaonesha kuwa wadatoga wote wanaopakana na Wairaqw wanazungumza Kiiraqw na zaidi ya nusu ya hao wadatoga wanajitmbulisha kama Wairaqw tena wengi wa hao wazazi wote wawili wakiwa wadatoga.
 
Baada ya kukaa Mama Isara kwa miaka mingi na baada ya sera ya serikali ya kikoloni ya Kiingereza kuamua kufyeka maeneo kuondokana na mbung`o waliokuwa wanasababisha tauni, Wairaqw walianza kutoka huko milimani na kujaza maeneo ya Karatu, Mbulu, Babati, Hanang na kusonga magharibi hadi Haydom kote huku wakisonga nyuma ya Wadatoga ambao huhamahama kutafuta malisho na ndio maana majina karibu yote ya huku yanaasili ya Kidatoga.
 
Je! jina Wairaqw ni Wambulu! na nini asili ya jina Mbulu? itaendelea kesho? 
 

No comments:

Post a Comment