Blog ya kijanja kwa ajili ya watu wajanja

Blog ya kijanja kwa ajili ya watu wajanja

Sunday, November 4, 2012

Mikoa vinara biashara ya binadamu yatajwa, Mkoa wa Singida ukiwemo

SHIRIKA la mtandao wa vijana linalojishughulisha na uzuiaji wa vitendo vya kikatili dhidi ya wanawake (Y2Y Movement), limeitaja mikoa ya Mara na Singida kuwa bado inakabiliwa na janga kubwa la vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake, ikiwa ni pamoja na biashara haramu ya kusafirisha binadamu.
 
Mbali na mikoa hiyo, mikoa mingine iliyotajwa kuendeleza vitendo hivyo vya kinyama, ni pamoja na Mwanza na Shinyanga, ambapo imeelezwa kwamba zaidi ya nusu ya wanawake na wasichana wamekuwa wakitendewa ukatili huo, huku asilimia 40 ya kundi la vijana wa kuanzia miaka 10 hadi 24 bado wanaamini kuwa mwanamke anayo haki ya kuteswa.
 
Akitoa mada katika semina ya kupambana na ukatili iliyofanyika jijini hapa, Mkurugenzi wa shirika hilo, Hellen Mahindi, alisema vijana wa mikoa ya Mara, Singida, Shinyanga na Mwanza wamekuwa wakijihusisha na ukiukwaji wa haki za binadamu kwa kumnyanyasa mwanamke.
 
Mahindi alisema baadhi ya jamii ya Mkoa wa Singida wamekuwa wakijihusisha na biashara haramu ya kusafirisha watoto wa umri mdogo kwenda mkoani Tabora kwa ajili ya kuwatumikisha katika baadhi ya shughuli, ikiwa ni pamoja na kutega na kufuga nyuki, kulima na kufanyishwa kazi ngumu za majumbani.
 
Aliitaka serikali kupitia vyombo vyake vya dola kufanya uchunguzi wa kina katika suala hilo, kisha hatua kali zichukuliwe mara moja kwa watu wote watakaobainika kuhusika na biashara hiyo haramu ya binadamu.
 
Alisema kuwa, lazima wanaharakati, mashirika na serikali washirikiane kwa pamoja kudhibiti hali hiyo na kujenga taifa lenye mtazamo chanya wa kimaendeleo.
 
“Asilimia 40 ya kundi la vijana bado wanaamini haki ya kunyanyaswa mwanamke. Hivi ni vitendo vibaya na tunatakiwa sote kwa pamoja tuunganishe nguvu kutokomeza kabisa ukatili wa namna hii, maana binadamu wote ni sawa,” alisema.
 
Mahindi alisema kuwa wamelenga kuhakikisha kuwa ifikapo mwaka 2015 asilimia kubwa ya vijana nchini watakuwa wameelimika na kuachana kabisa na unyanyasaji huu wa kijinsia.
 
Chanzo: Tanzania Daima Jumapili 04 Nov. 2012

No comments:

Post a Comment