Blog ya kijanja kwa ajili ya watu wajanja

Blog ya kijanja kwa ajili ya watu wajanja

Thursday, February 14, 2013

WALIMU WAPYA 26,537 WAAJIRIWA

WIZARA ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi imetoa ajira mpya kwa walimu 26,537 wa shule za msingi, sekondari na vyuo vya ualimu nchini.
 
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Waziri wa wizara hiyo, Dk. Shukuru Kawambwa, alisema kuwa utoaji wa ajira hizo haukufanyika kiholela bali ulifuata tathmini mbalimbali zilizofanyika kubaini maeneo yenye upungufu wa walimu ili kuwezesha kupeleka walimu kwa wingi katika maeneo hayo.
 
Waziri Kawambwa alisema kwa sasa taifa lina upungufu wa walimu wa masomo ya Sayansi na Hesabu na mwaka huu, wameajiri walimu 2,037.
 
Kwa mujibu wa Waziri Kawambwa, wameajiri walimu 13,568 wa ngazi ya cheti ambapo walimu 13,527 wamepangwa katika shule za msingi zilizopo kwenye halmashauri na 41 wamepangwa katika shule za mazoezi zilizo chini yake.
 
Alisema kwa upande wa wahitimu wa elimu ya shahada na stashahada, wameajiri walimu 12,893 kufundisha shule za sekondari zilizoko chini ya halmashauri, 59 wamepangwa kuwa wakufunzi wa vyuo vya ualimu, huku walimu 21 wamepangwa kufundisha shule za sekondari za mazoezi.
 
Aliongeza kuwa idadi hiyo ya walimu wenye shahada inajumuisha walimu 188 wa elimu maalumu ambao wamepangwa katika shule za sekondari na vyuo vinavyotoa elimu hiyo na kusema kuwa idadi ya walimu walioajiriwa mwaka huu imeongezeka kwa asilimia 11 sawa na walimu 2,630, ikilinganishwa na walimu 23,907 walioajiri mwaka uliopita.
 
Waziri huyo alisema kati ya walimu wa sekondari na vyuo waliochaguliwa, walimu 1,286 ni wale walioomba ajira serikalini kutoka soko la ajira ambao ni tofauti na wale wanaotoka vyuoni wakati walimu 841 walioshindwa mitihani mwaka jana, wamepatiwa ajira baada ya kurudia mitihani yao na kufaulu.
Alisema orodha ya majina na halmashauri walizopangwa, zinapatikana katika tovuti ya Wizara ya Elimu huku akitoa agizo kwa walimu waliohitimu ambao ni waajiriwa kurudi katika vituo vyao walivyokuwa wanafanyia kazi kabla ya kwenda masomoni.
 
Waziri Kawambwa alisema walimu wapya wanatakiwa kuripoti katika vituo vyao vya kazi Machi mosi hadi Machi 9, mwaka huu ambapo orodha ya mishahara yao ya mwezi huo itaingizwa katika utaratibu wa serikali.
“Walimu hao lazima waripoti ndani ya muda uliopangwa ili kuondoa usumbufu wa ulipaji mishahara na atakayeshindwa kufika, atakuwa amejitoa kwenye ajira hiyo,” alisema.
 
Alisema katika ajira hizo walimu wasishangae kupangiwa maeneo ambayo hawajayachagua kwani uteuzi wao umelenga maeneo yenye uhitaji zaidi huku akitolea mfano Mkoa wa Lindi ambao walimu wengi hukataa kwenda huko.
 
“Tumepanga kulingana na uhitaji, huwa tuna weka mwalimu mmoja kwa wanafunzi 46 lakini kwa hapa Dar es Salaam kuna walimu wengi na kufikia uwiano wa mwalimu mmoja kwa wanafunzi 20,” alisema.

Chanzo: Tanzania Daima

No comments:

Post a Comment