Blog ya kijanja kwa ajili ya watu wajanja

Blog ya kijanja kwa ajili ya watu wajanja

Tuesday, September 17, 2013

MCHINA WA NAPE MATATANI

CHADEMA yamshitaki balozi wa China nchini baada ya kushiriki mkutano wa CCM.  CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimemshtaki Balozi wa China nchini, Dk. Lu Youging kwa Umoja wa Mataifa (UN) kwa kujihusisha na siasa katika majukwaa nchini kitendo ambacho ni hatari katika uhusiano wa diplomasia kati ya Tanzania na China. Pia kimemshtaki kwa Serikali ya China na ya Tanzania kikidai kitendo cha balozi huyo ni kukiuka Mkataba wa Kidiplomasia wa Vienna (Vienna Convention of Diplomatic Reletions of 1964 ibara ya 41 (1-3) ambao unasimamia sheria za nchi wanachama w Umoja wa Mataifa. Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Chadema, Ezekiel Wenje alisema kitendo cha Balozi wa China, Dk. Youging kujihusisha na siasa za uenezi katika Chama cha Mapinduzi (CCM) ni kosa kubwa kimataifa na amepoteza sifa za kushikilia nafasi hiyo. Wenje ambaye pia ni Mbunge wa Nyamagana (CHADEMA) na Waziri Kivuli wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa alisema balozi huyo amevunja sheria za Mkataba wa Vienna ambao unasimamia sheria za nchi wanachama wa UN. Alisema kifungu alichovunja kinakataza Balozi yeyote kujihusisha na shughuli nyingine ambazo haziendani na majukumu ya uwakilishi wa nchi na nchi. Wenje alisema balozi huyo anapaswa kufikishwa kwenye vyombo vya sheria kama inavyoelekezwa katika mkataba wa Vienna kwamba ikiwa balozi atakiuka mkataba huo atakosa sifa na ataondolewa kinga aliyonayo na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria. Alisema: “Jambo hili katika macho ya diplomasia, limevunja misingi na taratibu za ushirikiano wa kimataifa, wenye nia njema kwa wananchi wa pande mbili, baina ya nchi na nchi na katika ngazi ya serikali. “Kwanza ni taswira ya dharau ya hali ya juu ambayo Balozi wa China ameamua kuwaonyesha Watanzania, hatuamini kwamba amepungukiwa na uwezo kiasi gani lakini anapaswa kukumbushwa aweze kuheshimu mipaka ya majukumu na wajibu wa diplomasia kwa nafsi ya balozi anapokuwa nchi ya ugenini. “Balozi huyu anapaswa kukumbushwa kuwa uhusiano wa vyama, kwa maana ya Chama cha Kikomunisti cha China na CCM hata kama ungekuwa mzuri kiasi gani hauna mwingiliano na uhusiano wa Serikali ya Tanznaia na China. “Hatutaki kuamini kuwa serikali ya China imemtuma Balozi Youquing kuja nchini kufanya kazi za ukatibu mwenezi wa CCM, tumesikitishwa heshima aliyopewa na Watu wa China ameidharau na amevuka mstari ambao hakuna mwanadiplomasia yeyote makini anayeheshimu uhusiano baina ya nchi na nchi angejaribu kufanya hivyo. “Mstari aliouvuka balozi huyu umefafanuliwa wazi katika Mkataba wa Vienna Convention wa 1961 hasa katika kifungu cha 41(1) na 3, katika masuala yanayohusu uhusiano na kinga za mabalozi, kwamba ni marufuku kwa mwanadiplomasia yeyote kuingilia siasa za ndani za nchi mwenyeji wake. “Chadema tunachukua hatua dhidi ya balozi huyo kujihusisha na chama cha siasa kwa kuvaa kofia ya CCM na kuelezea mambo ambayo hayakupaswa kusemwa kwenye majukwaa ya siasa. “Kwanza tunaandika barua tatu, moja itakwenda Serikali ya China, ya pili itakwenda UN na nyingine itakwenda Serikali ya CCM ambayo ndiyo imempeleka huko mikoani. “Barua hizo zitakuwa zinataka kueleza msimamo wa tukio hilo la balozi wa China nchini kujihusisha na siasa za majukwaani na kuvaa nguo za CCM, tunataka kujua hatua gani zitakazochukuliwa haraka kabla ya Chadema hatujapendekeza hatua za kuchukua. “Hii ni hatari kwa balozi huyo kujiingiza kwenye siasa kitendo kinachosababisha kuhatarisha uhusiano uliopo kati ya wawekezaji wa China nchini kwa sababu wananchi wanaweza kutafsiri vibaya. “Kwa mfano kuna maeneo ni ngome za Chadema na pale kuna wawekezaji wa China wanaweza kukataa kutoa ushirikiano wakidai ni wapo mlengwa wa CCM, pia ni hatari chama kingine kitapokuja kushika dola hakutakuwa na uhusiano mzuri. “Tutaambatanisha ushahidi wa kutosha katika barua hizo ikiwa ni pamoja na picha za mnato na video, maneno aliyotamka kwenye mkutano, picha inayoonyesha akiwa amveaa sare za CCM na jinsi anavyocheza”. Picha zilizonyeshwa kwa waandishi wa habari zilionyesha Balozi Youging akiwa katika mikutano mbalimbali ya CCM maeneo ya Kishapu, Shinyanga na Kahama. Katika picha hizo balozi huyo alionekana amevaa sare za CCM, akihutubia na kuendesha baiskeli akiwa na viongozi wa chama hicho akiwamo Katibu Mkuu, Abdulrahman Kinana, Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye. Kwa mara ya kwanza balozi huyo aliibukia katika mkutano waCCM uliofanyika Shinyanga huku akishangiliwa na wananchi alipojaribu kuzungumza kisukuma. CCM yazungumza Wakati huohuo Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimesema kimesikitishwa na hatua ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kumshutumu Balozi wa China, Dk. . Lu Youqing kwa kuhudhuria mikutano ya CCM. Kimewataka watanzania kupuuza madai ya Chadema kikisema hayana msingi kwa maendeleo ya taifa na watu wake. Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye alikuwa akizungumza na waandishi wa habari katika mkutano uliofanyika katika Kijiji cha Mwandoya wilayani Meatu. Alisema ni wazi Chadema kinataka kutumia matatizo ya wananchi kuyageuza agenda ya siasa. Chadema haina budi itambue kuwa chama tawala cha China (CPC) kimekuwa na urafiki wa muda mrefu na CCM ikizingatia Balozi Dk. Lu pia ni kiongozi wa chama hicho. Nape alisema hatua ya Balozi huyo kuhudhuria mkutano huo ni mafanikio ya ziara ya iliyofanywa na Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana China mapema mwaka huu. “Balozi Dk. Lu amekuja kuleta ukombozi kwa watanzania hasa wa Kanda ya Ziwa kwa kuleta wawekezaji katika Mkoa wa Shinyanga kwa kujenga viwanda wa nyuzi, pamba, nyama, maji na ngozi ambako ajira zaidi ya 1000 zitapatikana. “Watanzania wapuuze madai haya kwani si dhambi kwa Balozi wa China kuhudhuria mkutano wa CCM… urafiki wetu hakuanza leo ni wa muda mrefu katika historia ya nchi hizi mbili tangu na baada ya Uhuru,” alisema Nape. Nape alisema CCM imepitaka kila eneo la yakiwamo majimbo yanayoongozwa na wapinzani na kubaini kuwapo changamoto nyingi. Aliitaka Chadema kwenda kutatua haraka matatizo hayo badala ya kufanya mikutano Dar es Salaam pekee. Wiki iliyopita akiwa mjini Shinyanga Balozi Dk. Lu Youqing, alihudhuria mikutano ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kusema kuwa hakuna chama imara kama hicho. -MtanzaniaCHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimesema kuwa Balozi wa China nchini, Lu Youqing, amekiuka mkataba wa kimataifa wa Vienna kwa kuanza kushiriki kazi ya uenezi wa Chama cha Mapinduzi (CCM) kama alivyoonekana akiwa mkoani Shinyanga.
 
Wakati CHADEMA ikitoa madai hayo, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa imekiri balozi huyo kuvunja mkataba huo unaoongoza uhusiano wa kidiplomasia na kuahidi kuchukua hatua.
 
Septemba 12 mwaka huu, balozi huyo alihudhuria mkutano wa hadhara wa CCM uliofanyika uwanja wa Shycom mkoani Shinyanga na baadaye katika eneo la mnada wa Mhunze Jimbo la Kishapu.
Balozi Youquing alitambulishwa kwa wananchi na Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana, na kisha kuwahutubia akisema China imevutiwa na sera za CCM na hivyo itawekeza katika soko la pamba katika mkoa huo.
 
Ni katika mkutano huo, balozi huyo alicheza nyimbo za CCM za kubeza vyama vya upinzani huku akiwa amevalia kofia ya chama hicho.
 
Akizunguza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Mambo ya Nje wa CHADEMA, Ezekia Wenje, alisema balozi huyo amekiuka mkataba wa kimataifa wa Vienna kuhusu mambo ya kidiplomasia kifungu cha 41 (i).
 
Alisema kifungu hicho kinakataza mabalozi wa nchi kujiingiza katika masuala ya ndani ya nchi nyingine.
 
Wenje alibainisha kuwa mkataba huo unataka kazi za balozi kuwa ni kuwakilisha nchi na si chama.
“Balozi wa China yuko hapa kuwakilisha China nchini Tanzania, si Chama cha Kikomunisti kwa CCM,” alisema.
Wenje aliongeza kuwa haamini kama huo ndio msimamo wa serikali ya China na pia CCM kwani Waziri wa Mambo ya Nje, Bernard Membe, alinukuliwa akiwaonya mabalozi kuingilia mambo ya ndani ya nchi kwa nyakati tofauti wanapokuwa wameongea na vyama vya upinzani.
 
Alisema kuwa CHADEMA imeazimia kuiandikia barua serikali ya China ili kuweza kupata msimamo wake kwa tabia ya balozi huyu kuandamana na chama kimoja na kutumia vifaa vyake vya uenezi katika mikutano ya hadhara.
 
Aliongeza kuwa wataiandikia pia serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kuomba ufafanuzi wa jambo hili na pia kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ambaye ndiye msimamizi halali wa mkataba wa Vienna.
 
Naye Mkurugenzi wa Bunge na Hamashauri wa CHADEMA, John Mrema, alisema tabia hiyo inahatarisha uhusiano wa China na Tanzania endapo CHADEMA au chama kingine kitaingia madarakani.
 
Mrema Aliongeza kuwa kitendo hicho kinaongeza mazingira hatari kwa wawekezaji wa Kichina waliopo nchini hasa kwenye maeneo ambayo CCM haikubaliki.
 
Mkurugenzi wa Mafunzo na Oganaizesheni, Benson Kigaila naye alisema kuwa wanawashangaa CCM kwa kuwa wanafanya mzaha na kila kitu.
 
“Wametumia wafanyakazi wa serikali katika siasa kwa muda mrefu bila mafanikio hadi wameanza kutumia mabalozi ili waweze kukubalika kwa wananchi,” alisema.
 
 
CCM wajitetea
 
 

Alipotafutwa Katibu wa Halmashauri Kuu (NEC) Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alisema kuwa ziara ya balozi huyo mkoani Shinyanga haikuwa ya kisiasa bali ilitokana na mazungumzo kati ya chama hicho na Chama cha Kikomunisti cha China.
 
Alisema kuwa lengo lilikuwa ni China kuweza kuwekeza katika kilimo cha pamba na mifugo kuongeza ajira.
 
“Katika suala hilo CCM ilikuwa nyuma ya kuhamasisha wawekezaji, Katibu wetu alipokwenda China aliomba wawekezaj na watawekeza katika viwanda kumi na sasa wameanza na vitatu, ndio sababu Balozi wa China alienda kumwonyesha Kinana.
 
Nape aliongeza kuwa balozi huyo alipita katika mkutano wa hadhara na kuomba kusalimia wananchi kuelezea uwekezaji utakaofanywa na China.
 
“CHADEMA kulalamika ni kwamba wameweweseka kwa kuwa wamezoea kutumia matatizo ya wananchi kama mtaji wa kisiasa, tatizo la bei ya pamba likiendelea ni mtaji kwao na likiisha watakosa mtaji wa kisiasa,” alisema.
 
Wizara yacharuka
Waziri wa Mambo ya Nje, Bernard Membe, hakupokea simu yake kufafanua suala hilo lakini alipoandikiwa ujumbe na kupigiwa tena simu ilipokelewa na msaidizi wake ambaye aliahidi kutuma taarifa.
 
Kwa mujibu wa taarifa hiyo iliyotolewa na Togolani Mavura kwa niaba ya Waziri Membe ilisema kuwa imefuatilia suala hilo kwenye vyombo vya habari kuhusu kushiriki kwa Balozi wa China nchini kwenye mkutano wa hadhara wa CCM.
 
“Taarifa hizo zimeambatana na picha zinazomuonyesha balozi huyo akiwa amevaa kofia yenye nembo ya CCM. Habari zinaeleza kuwa alikwenda Shinyanga kuhudhuria uzinduzi wa mradi wa viwanda vya kuchambulia pamba vinavyojengwa na mwekezaji wa Kichina anayeitwa Tahong.”
“Viwanda hivyo vitakuwa na uwezo wa kuchambua tani 120,000 za pamba kwa mwaka, vitakapokamilika mwakani,” alisema.
 
Aliongeza kuwa wizara inapenda kutamka kwamba kitendo cha balozi yeyote kuhudhuria mikutano ya hadhara ya vyama vya siasa na kuvaa sare zenye nembo ya vyama sio sahihi.
 
Ni kukiuka kifungu cha 41(1) cha mkataba wa Vienna wa mwaka 1961, unaoongoza uhusiano wa kidiplomasia.
 
“Katika kipindi cha mwaka 2010 hadi 2012 wizara ilikumbana na vitendo vinavyofanana na kitendo hiki na ikachukua hatua stahiki.
 
“Kadhalika kwa tukio hili, waziri anakusudia kuchukua hatua za kidiplomasia zinazostahili ili kuzuia jambo hili lisitokee tena,” alisema.
 
Via - Tanzania Daima

No comments:

Post a Comment